The House of Favourite Newspapers

Tuhuma Nzito…. Daktari ‘Muuaji’

0

HII ni tuhuma nzito kwa tasnia ya udaktari! Aliyekuwa daktari maarufu ambaye pia alikuwa anamiliki kliniki anadaiwa kuua wanawe wawili kwa kuwadunga sindano ya sumu aina ya insulini.

 

Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Nakuru nchini Kenya, Beatrice Kiraguri amethibitisha kisa hicho, lakini akakataa kumtaja daktari huyo.

 

Alisema baada ya kufanya mauaji hayo, daktari huyo analazwa katika Hospitali Kuu ya Mkoa wa Bonde la Ufa chini ya usalama mkali wa Polisi kufuatia naye kufanya jaribio la kujiua.

 

“Hatuna uhakika ni dawa gani ambayo watoto walidungwa na ambayo inaweza tu kudhibitishwa kupitia uchunguzi wa maiti baada ya uchunguzi wa miili,” alisema.

 

Aliongeza kuwa suala hilo lilikuwa likiendelea kuchunguzwa ili kuthibitisha ikiwa ni daktari aliyefanya kosa hilo.

“Mke wa daktari hakuwa nyumbani wakati huo na aliitwa tu wakati watoto walikuwa tayari wamekufa,” Beatrice alisema bila kusema ni nani aliyemwita.

 

Alisema kuwa, Polisi walilazimika kuvunja nyumba hiyo kujaribu kuwaokoa watu watatu, lakini watoto walikuwa wameshaaga dunia.

Jirani alidai kwamba daktari huyo alichukua hatua kali baada ya kutokubaliana na mkewe ambaye anadaiwa alitaka kusafiri nje ya nchi kinyume na mapenzi yake.

 

Miili ya watoto hao ilipelekwa katika chumba cha kuhifadhi maiti cha Kaunti ya Nakuru.

Hata hivyo, kwa mujibu wa mashuhuda, daktari huyo anajulikana kwa jina la James Gakara ambaye alikutwa amelala kando ya wanawe akiwa amepoteza fahamu katika kisa ambacho anashukiwa kutekeleza mauaji na kujaribu kujiua.

 

Kwa mujibu wa ripoti mbalimbali za vyombo vya habari nchini humo, Gakara ambaye amekuwa akipokea matibabu katika Hospitali ya Nakuru Level Five, alipumua pumzi yake ya mwisho Septemba 22, mwaka huu kisha naye aliaga dunia.

 

Gakara; daktari wa wanawake mjini Nakuru, anatuhumiwa kumuua Dylan Gakara mwenye umri wa miaka mitano na Karuana Gakara mwenye umri wa miaka mitatu, kabla ya kujaribu kujitoa uhai katika makazi yake ya Kiamunyi Estate huko Nakuru.

 

Inaripotiwa kuwa baada ya daktari huyo kurejesha fahamu, alikiri kuwaua malaika hao kwa kuwachoma sindano ya insulin.

Hata hivyo, dada wa Daktari James Gakara, Mary Gakara amesema kwamba kaka yake aliwapenda mno watoto wake na hangejaribu wala kufikiria kuwaua hata kwa sekunde.

 

“Namfahamu sana kaka yangu, sidhani angefanya kitendo kama hicho, ninachojua angefanya kila awezalo kuwalinda watoto wake, hakuwa mtu ambaye ungedhani angeweza kumuua mtu,” anasema Mary mbele ya vyombo vya habari.

 

Hata hivyo, habari nyingine zilieleza kuwa, mke wa daktari huyo, Winnie Odhiambo kwa uchungu, aliwaombolezea wanawe na akijutia kuwa hakuwalinda vya kutosha.

 

“Moyo wangu umevunjika. Nilishindwa kuwalinda wapendwa wangu. Mtu ambaye mlimuamini sana aliwasaliti, naahidi kupigania haki yenu wapendwa wangu,” alisema mama huyo katika tukio hilo ambalo limevuta hisia za wengi.

STORI; BAKARI MAHUNDU, DAR

Leave A Reply