Baada ya Kutokuelewana kwa Miaka Miaka Kadhaa, Hatimaye Diamond, Baba’ke Wapatana
STORI: GLADNESS MALLYA NA MUSA MATEJA | Gaztei la Risasi Jumamosi, Toleo la Desemba 24, 2016
DAR ES SALAAM: Hakuna marefu yasiyokuwa na ncha katika dunia hii ya duara! Baada ya kutofautiana kwa muda mrefu na baba yake, mzee Abdul Jumaa, hatimaye staa wa Afro-Pop, Nasibu Abdul Jumaa ‘Diamond Platnumz’, amepatana na mzazi wake huyo.
Habari za uhakika kutoka kwenye chanzo cha kuaminika katika familia ya Diamond zilieleza kuwa, hivi karibuni staa huyo na baba yake waliamua kupotezea maneno ya watu na kwamba wafanye wafanyavyo kuhakikishia kuwa wanamaliza tofauti zao hivyo kwa sasa wanajuliana hali kama baba na mtoto au mtoto na baba na kushirikishana katika mambo yao.
“Unajua kati ya vitu alivyokuwa akivitamani Diamond ni kuwa vizuri na mzee (baba Diamond) na hicho ndicho kilichofanyika.
“Kizuri zaidi ni kwamba, baba Diamond amekuwa akimuomba Diamond msamaha na kujutia kosa lake (kumtelekeza na mama yake, Sanura Kassim ‘Sandra’ tangu akiwa mdogo) kwa hiyo Diamond akaona bora amsamehe na kusahau yaliyopita kwani si ndwele badala yake wagange
mapya.
Baba Diamond
AANZA KUMTUMIA HELA
“Kwanza katika kuthibitisha kwamba wapo vizuri, Diamond alianza kwa kumjulia hali baba yake hasa juu ya kuumwa kwake kisha kumtumia hela ndogondogo za matumizi tofauti na zamani maana katika kuomba msamaha, baba Diamond alimuomba sana amsaidie kutokana na kusumbuliwa na ugonjwa wa miguu na hali ya kimaisha kuwa si nzuri kiivyo.
“Mbali na hivyo, pia amemuwekea utaratibu wa kumpa mtonyo kila mwezi ili naye afaidi matunda ya mwanaye.
“Kinachoonekana kila mmoja aligundua kosa lake au aliwekwa chini na kukubaliana kabisa kwamba mwenendo wa mgogoro kati ya baba na mtoto au mtoto na baba hautawaacha salama.
“Kuna waliosema kitendo cha Diamond kumtenga baba yake kilikuwa kinampeleka kwenye laana lakini wengine walisema manung’uniko yake kuwa baba yake alimtelekeza nayo yasingemuacha baba Diamond salama hivyo kupatana kwao ni jambo kubwa mno kwenye maisha yao na hata mashabiki wa Chibu (Diamond) watafurahi kwamba kwa sasa yupo vizuri na mshua wake,” kilifunguka chanzo hicho kwa sharti la kutotajwa gazetini hata kwa mtutu wa bunduki.
HUYU HAPA BABA D
Baada ya kuinyaka ishu hiyo,
gazeti hili lilianza kwa kumsaka baba Diamond ambaye alipopatikana nyumbani kwake, Magomeni-Kagera jijini Dar alithibitisha kupatana na mwanaye huyo na kwamba muda mfupi baadaye alimwambia mwandishi wetu kuwa ana safari ya kwenda nyumbani kwa Diamond, Madale-Tegeta, Dar.
“Watu wanaposema kuwa Diamond hanisaidii kwa sasa hivi hawajui ukweli. Ukweli ni kwamba mimi ananisaidia na hatuna tatizo lolote.
“Kwanza hapa nina safari ya kwenda Madale kwa hiyo kama una nafasi twende wote,” alisema baba Diamond akionesha sura ya nuru na bashasha.
HADI MADALE
Hata hivyo, kama alivyoomba, mwandishi wetu aliambatana na baba Diamond hadi Madale na kushuhudia akitinga ndani huku mwandishi wetu akiishia getini baada ya kuzuiwa na walinzi.
Akiwa nje ya nyumba hiyo, mwandishi wetu alimshuhudia baba Diamond akiwa kwenye pilika mbalimbali akiingia na kutoka kwenye nyumba hiyo akionekana mwenye uzoefu maeneo hayo kutokana na namna alivyokuwa akisalimiana na majirani.
Uchunguzi wa gazeti hili, ulibaini kuwa wakati baba Diamond akijiachia kwa mwanaye huyo, wenyeji wake hasa mwanaye Diamond, mama Diamond na mkwewe Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’ hawakuwepo.
DIAMOND AJIBU KWA KIFUPI
Gazeti hili lilipomtafuta Diamond na kumuuliza juu ya suala hilo alijibu kwa kifupi: “Mimi na mzee tupo fresh tu hamna tatizo.”
Mamam Diamond
MAMA DIAMOND VIPI?
Kwa upande wake mama Diamond hakupatikana nyumbani kwake, Tandale wala Madale kwa maelezo kuwa yupo nchini Afrika Kusini akimlea mjukuu wake mpya lakini huko nyuma aliwahi kukaririwa na gazeti hili akizungumzia mtafaruku wa Diamond na baba yake:
“Huwa ninaumia kwani Diamond kila mwezi huwa anapeleka hela ya matumizi kwa baba yake, sasa sijui maneno kuwa wana ugomvi yanatoka wapi? Ninachojua kwa sasa hawana shida kabisa na mambo ni poa.”
Gaztei la Risasi Jumamosi, Toleo la Desemba 24, 2016
HUKO NYUMA
Diamond na baba yake wamekuwa kwenye mgogoro wa muda mrefu ambapo mzazi huyo alikuwa akilalamika kwamba mwanaye huyo hakuwa akimjali na hata alipokuwa akijaribu kumpigia simu alikuwa hampi ushirikiano.
Kwa upande wake Diamond amekuwa beneti na mama yake kwa madai kuwa baba yake huyo alimtelekeza baada ya kutengana na mama yake kisha akaoa mwanamke mwingine lakini sasa ‘mambo ni kama Ulaya mwanangu’.
Comments are closed.