The House of Favourite Newspapers

Basata Yafunguka Kuhusu Jeneza na Msalaba wa TundaMan Baada ya Kupokea Malalamiko

0
TundaMan akitumbuiza katika Tamsha la Simba Day

BARAZA la Sanaa la Taifa (BASATA) limekanusha taarifa za kumfungia msanii wa Bongo Fleva, Khalid Ramadhan maarufu kama Tunda Man ingawa wanachunguza malalamiko waliyopokea kutokana na matumizi ya jeneza na msalaba alivyoingia navyo msanii huyo wakati wa kutumbuiza kwenye Tamasha la Simba Day, Jumatatu, Agosti 8, 2022.

 

Katibu Mtendaji wa BASATA, Dkt Kedmon Mapana amesema taasisi hiyo haipo kwa ajili ya kuwafungia wasanii bali kuwasimamia na kuwaelekeza namna bora kufanya ubunifu wa kiushindani katika kazi zao.

 

“Taarifa na sisi tunaziona kwenye mitandao ya kijamii kwamba tumemfungia msanii, lakini sisi kama BASATA hatujamfungia msanii yeyote, kilichopo hapa kwetu ni kuhusu matumizi ya jeneza na Zaidi ni kuhusu matumizi ya msalaba.

 

“Inaonekana upande wa Wakristo kuna hayo malalamiko yanaendelea na sisi tumeshayapata, tunaendelea kuyafanyia kazi, tutakapokamilisha basi tutatoa tamko.

 

“Lakini kwa sasa hatujamfungia msanii yeyote na wanaoandika kwamba BASATA imemfungia mtu, natoa tahadhari, yawezekana wanaona BASATA ni Baraza la kufungia tu, lakini sisi hatutaki kufungia, kazi yetu ni kuwaeleza wasanii wawe wabunifu, wafanye Sanaa kwa umakini.

 

“Kabla hujatoka huko ujiulize, hivi mimi nikitoka na huu msalaba, mwenzangu huko atanielewa vipi? Kwa hiyo wasanii wanapaswa kujiuliza maswali kabla ya kwenda kwenye hadhira yao, nah ii itatusaidia sana. Lazima tukusanye maoni ya watu wanasema nini, tukikamilisha tiutaoa taarifa,” amesema Mapana.

Leave A Reply