The House of Favourite Newspapers

Benchi la Ufundi Kuvunjwa Simba, Matola Anukia

0

IMEFAHAMIKA kuwa wakati wowote Klabu ya Simba itaachana na benchi zima la ufundi huku tetesi zikimtaja kocha wa sasa wa Polisi Tanzania, Suleiman Matola anaweza kurejea ‘nyumbani’ kuwa kocha msaidizi wa timu hiyo.

 

Hiyo imekuja ikiwa ni saa chache kabla ya kikao cha Bodi ya Wakurugenzi ya klabu hiyo ikitarajiwa kukutana jana usiku na kocha Mbelgiji, Patrick Aussems kuzungumzia hatima yake kwenye timu hiyo iliyo chini ya Denis Kitambi hivi sasa.

 

Ni mara ya pili mfululizo kwa Matola kutajwa kwenye misimu miwili ya hivi karibuni, awali ilikuwa kwenye msimu uliopita kabla ya Kitambi kupewa nafasi hiyo ya kocha msaidizi.

 

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Ijumaa kutoka ndani ya bodi ya timu hiyo muda wowote klabu hiyo itatangaza kuachana na benchi zima la ufundi.

 

Mtoa taarifa alisema kuwa Matola ndiye aliyepewa nafasi kubwa ya kufundisha timu hiyo baada ya kuwapita makocha wengine wazawa ambao majina yao yalikuwepo mezani yakijadiliwa.

 

Aliongeza kuwa mara baada ya Matola kutangazwa, haraka atajiunga na timu hiyo kwa ajili ya kuifundisha huku viongozi wakiendelea kumtafuta kocha mkuu atakayeungana na Matola.

 

“Ni suala la muda hivi sasa juu ya Matola kutangazwa kuwa kocha msaidizi hiyo ni baada ya vikao vya bodi ya klabu kumpitisha kuwa kocha msaidizi, ni baada ya benchi kupanga kuvunjwa.

 

“Kocha Mkuu ambaye ni Aussems leo (jana) usiku alitarajiwa kukutana na viongozi wa bodi ya klabu kwa ajili ya kuzungumzia hatima yake, pia kufikia hatima nzuri kabla ya kumpatia barua ya kuachana naye.

 

“Hivyo, baada ya kikao hicho haraka viongozi watamtangaza Matola kuwa kocha msaidizi wa Kitambi huku mabosi wakiendelea na mchakato wa kumtafuta kocha mkuu,” alisema mtoa taarifa huyo na kuongeza:

 

“Viongozi juzi walikasirishwa na kitendo kibaya alichokifanya Kitambi cha kuzungumzia masuala ya timu mara baada ya mazoezi akisema kuwa yeye ndiye kocha hivi sasa baada ya Aussems kusimamishwa.

 

“Kauli hiyo inamaanisha kuwa siyo msiri kutokana na kutoa siri za timu, hivyo baada ya kauli hiyo haraka viongozi walimuita na kukaa naye kikao na kumpa onyo la kutorudia tabia ya kuongea hovyo kwenye Vyombo vya Habari.”

Wilbert Molandi, Dar es Salaam

SPOTI HAUSI: ZAHERA ni MALI ya SIMBA Kwa SABABU Hii / SAMATTA Amfunika MO SALAH..

Leave A Reply