The House of Favourite Newspapers

Benki ya NBC, Jubilee Allianz Kutoa Huduma za Bima Kupitia Vituo vya Total Energies

0
Mkurugenzi wa Wateja wadogo na Binafsi wa Benki ya NBC Elibariki Masuke  (wa pili kulia) sambamba na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Bima ya Bima ya Jubillee Allianz Bw Dipankar Charya (kulia), Mkurugenzi wa Sheria na Uhusiano wa Kampuni ya mafuta ya Total Energies, Bi Getrude Mpangile ( wa pili kushoto) na Mkuu wa Idara ya Bima kupitia benki wa Benki  ya NBC Bw  Benjamini Nkaka (kushoto) wakionesha nembo maalum yenye jina la kampeni maalum inayofahamika kama ‘Bima Mazima’ inayotoa fursa kwa wamiliki wa vyombo vya usafiri hususani  wanaoishi jijini Dar es Salaam kupata huduma mbalimbali za kibima kupitia baadhi ya vituo vya mafuta vya kampuni ya Total Energies. Hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyi imefanyika hii leo jijini Dar es Salaam.

Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) kwa ushirikiano na Kampuni ya Bima Jubilee Allianz wamezindua kampeni maalum inayofahamika kama ‘Bima Mazima’ inayotoa fursa kwa wamiliki wa vyombo vya usafiri hususani  wanaoishi jijini Dar es Salaam kupata huduma mbalimbali za kibima kupitia baadhi ya vituo vya mafuta vya kampuni ya Total Energies.

Ushirikiano huo unatajwa kwamba unalenga kurahisisha upatikanaji wa huduma ya bima kwa watumiaji wa vyombo hivyo ambapo wamiliki watapata huduma hiyo kwa urahisi katika vituo vya Total Energies ambavyo kupitia mpango huo vinatambulika kama mawakala wa bima wa benki ya NBC yaani ‘NBC Bancassurance Agency’

Hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyo imefanyika mapema hii leo jijini Dar es Salaam ikihudhuliwa na wadau mbalimbali wa mpango huo wakiwemo maofisa waandamizi pamoja na wafanyakazi wa benki ya NBC, Total Energies, Jubilee Allianz pamoja na wateja.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Mkurugenzi wa Wateja wadogo na Binafsi wa Benki ya NBC Elibariki Masuke  aliemuwakilisha Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya NBC, Theobald Sabi alisema ushirikiano huo unalenga kutoa ulinzi dhidi ya hasara na uharibifu unaosababishwa na ajali, ikiwa ni pamoja na moto, kugongana, na kupinduka kwa vyombo hivyo.

Mkurugenzi wa Wateja wadogo na Binafsi wa Benki ya NBC Elibariki Masuke  (kulia) sambamba na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Bima ya Bima ya Jubillee Allianz Bw Dipankar Charya (katikati) pamoja maofisa wengine wa kutoka taasisi hizo wakifuatilia uzinduzi wa kampeni hiyo.

“Tunaamini kwamba kupitia ushirikiano huu wa NBC, Total Energies na Jubilee Allianz tunakwenda kutoa huduma ya bima stahiki kwa gharama nafuu na kuleta ahueni kwa wamiliki wa vyombo vya moto dhidi ya majanga mbalimbali yanayowakumba,’’ alisema

Zaidi Bw Masuke alibainisha kuwa NBC kupitia bidha ya Insurance Premium Financing yaani IPF (NBC Mkopo Bima), pia itashirikiana na Total na Jubilee Allianz kuhakikisha kuwa wteja wanapata bima hata pale ambapo wanakua hawana kiasi kamili cha kununua bima kwa wakati mmoja.

Mmoja wa watoa huduma wa kampuni Kampuni ya mafuta ya Total Energies akitoa huduma ya Bima kwa mmoja wa wateja wa kituo hicho Bw Ally Nchahaga (alieketi ndani ya gari) akiwa ni mteja wa kwaza baada ya uzinduzi wa kampeni maalum inayofahamika kama ‘Bima Mazima’ inayotoa fursa kwa wamiliki wa vyombo vya usafiri hususani  wanaoishi jijini Dar es Salaam kupata huduma mbalimbali za kibima kupitia baadhi ya vituo vya mafuta vya kampuni ya Total Energies. Kampeni hiyo inaratibiwa na Benki ya NBC kwa kushirikiana na kampuni ya Bima ya Bima ya Jubillee Allianz na kampuni ya Total Energies.  Hafla ya uzinduzi wa kampeni hiyi imefanyika hii leo jijini Dar es Salaam.

“Bidhaa hii inatoa fursa kwa wamiliki wa magari kupata Bima na kuilipia kwa awamu 4  hadi 10 huku wakipata usalama/ ulinzi wa bima stahiki dhidi ya majanga. Zaidi, katika kipindi hiki cha kampeni wateja  watapata huduma ya ukaguzi wa gari bure na wamiliki wenye bima za gharama kuanzia TZS 400,000 kupitia Jubilee Allianz watapata huduma ya msaada wa barabarani (towing) na ‘jump start’ bure wanapofikwa na majanga haya.’’ alibainisha

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Bima ya Jubillee Allianz Bw Dipankar Charya alisema ushirikiano huo pia unajumuisha Bima ya Ajali, inayotoa faida za kifedha kwa dharura za kujeruhiwa, kudhurika, au kifo kutokana na ajali zinazohusisha njia mbalimbali za usafiri, ikiwa ni pamoja na mabasi, treni, ndege, pikipiki, na bajaji.

Alitaja aina ya bima zinazotolewa kupitia mpango huo kuwa ni pamoja na bima ya ‘Comprehensive Insurance’ inayotolewa kwa asilimia 3.5 ya thamani ya gari na  kiasi cha sh 118,000 kwa bima ya ‘third party’.

‘’Kwa wateja wenye Mfumo wa Kufuatilia vyombo vyao (GPS Tracking System) watapata punguzo la 5% kwenye gharama za bima.’’ Alibainisha.

Akizungumza kwenye hafla hiyo Mkurugenzi wa Sheria na Uhusiano wa Kampuni ya Total Energies, Bi Getrude Mpangile alisema kampeni hiyo ya miezi mitatu itahusisha vituo vya Total Energies vilivyopo Oysterbay, Morocco, Mlimani City, Kariakoo na Samora.

 

“Siku zote dhamira yetu Total Energies ni kurahisisha huduma kwa wateja wetu. Ni kupitia dhamira hiyo ndio maana mara kwa mara tunajitahidi kuongeza huduma mbalimbali za kijamii na kibiashara kwenye vituo vyetu ili wateja wetu wanapofika hapa wasiishie tu kununua mafuta bali pia wanapata vilainishi vya magari yao, wanapata huduma ya ‘service’ ya magari ikiwemo kuoshewa magari na pia huduma nyingine zikiwemo za kifedha, supermarkets na hii mpya ya bima’’ alitaja.

Leave A Reply