The House of Favourite Newspapers

Biashara Yatua leo Addis Ababa, Uzembe Watajwa

0
Kikosi cha Biashara Utd kilivyotua katika Uwanja wa ndege wa Addis Ababa Ethiopia leo Alfajiri.

LEO Ijumaa kikosi cha Biashara United kinatarajiwa kushuka dimbani kwenye mchezo wa hatua ya awali ya michuano ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Dakhil FC ya Djibouti.

 

Hadi juzi Jumatano kikosi cha Biashara kilishindwa kusafiri kutokana na kuchelewa kwa hati za kusafiria pamoja na Visa jambo ambalo liliwalazimu kuondoka jana Alhamisi zikiwa zimebaki saa chache kabla ya mchezo wenyewe kupigwa.

 

Biashara United inashiriki michuano hii kwa mara ya kwanza tangu ipande daraja msimu wa 2018/19 na hii ni baada ya timu hiyo kumaliza kwenye nafasi nne za juu msimu uliopita.

 

Ratiba ya michuano ya kimataifa kwa timu zinazoshiriki Kombe la Shirikisho na michuano ya Ligi ya Mabingwa ilitoka takriban Majuma matatu yaliyopita hivyo kulikuwa na muda mwingi kwa timu shiriki kufanya maandalizi mapema kuhakikisha wanashugulikia changamoto zote ambazo zinawakabili.

 

Jambo la kushangaza ni kuona uongozi wa Biashara United unahaha kutafuta vibali pamoja na hati za kusafiria za wachezaji zikiwa zimebaki siku chache kabla ya timu kusafiri.

 

Wakati ligi imemalizika ulikuwa ni muda muafaka kwa uongozi kuanza mchakato wa mapema na mambo kama haya yasingejitokeza wakati timu ikiwa katika hatua za mwisho kusafiri.

 

Kwa timu kama Biashara ambayo inashiriki michuano hii kwa mara ya kwanza isingekuwa dhambi kwa viongozi kuuliza kwa viongozi wa timu ambazo zimekuwa na uzoefu wa kusafiri kwenye michuano hii ya kimataifa kuona ni vitu gani walitakiwa kuvikamilisha kwa wakati lakini haikuwa hivyo.

 

Kikosi kimesafiri jana mchana na kimewasili Djibouti leo Alfajiri ambapo saa 10:00 Alasiri watashuka dimbani kucheza mechi yao, kiufundi hapa unaona Biashara wanahitaji miujiza ili waweze kuibuka na ushindi kwani ni wazi wachezaji wataingia kwenye mchezo huu wakiwa na uchovu kutokana na kusafiri umbali mrefu hivyo ilikuwa ni lazima wapate muda wa kupumzika ili kurudisha miili kwenye hali yake ya kawaida baada ya safari ndefu.

 

Wanapaswa kutambua kuwa nafasi nne za kushiriki kimataifa hazijaja kwa ngekewa kuna timu zimepambana hadi nafasi hizi zimepatikana hivyo timu ambazo zinapata nafasi ya kushiriki michuano hii zinapaswa kutambua kuwa wana jukumu zito la kuhakikisha nafasi hizi tunazilinda ili zisiende kwingine.

 

Mashindano ya kimataifa hayataki ujanja ujanja ambao hauna kichwa wala miguu bali yanahitaji maandalizi ya kutosha na utayari wa kutosha kuanzia ndani hadi nje ya uwanja, hili la Biashara liwe fundisho kwa timu nyingine ambazo zitapata nafasi ya kushiriki michuano mbalimbali ya kimataifa.

 

Ni wazi viongozi wa Biashara United wanapaswa kukubali lawama hizi kwani wao ndiyo sababu kubwa kwa kikosi chao kushindwa kusafiri kwa wakati na endapo watashindwa kupata matokeo kwenye mchezo wa leo wanapaswa kujilaumu wenyewe.

Leave A Reply