Diwani Obama Aahidi Sekondari yake iliyoshika Mkia Dar, kuwa Yakwanza
Diwani wa Kata ya Mabwepande Dar, Muhajirina Kassim Obama ambaye shule ya kata yake Mabwepande Sekondari imeshika mkia katika matokeo ya kidato cha nne mwaka jana ameahidi kuisimamia shule hiyo na kuwa ya kwanza badala ya mwisho.
Diwani Obama alisema hayo mwishoni mwa wiki iliyopita alipofanya ziara kwenye shule hiyo na kukutana na wazazi, walimu na kamati ya maendeleo ya shule hiyo.
Katika ziara hiyo diwani Obama alisikiliza maoni ya wazazi, walimu na wanafunzi wa shule hiyo na kubaini changamoto nyingi zilizopelekea shule hiyo kushika mkia katika mkoa wa Dar.
Akizungumza katika ziara hiyo diwani Obama amesema katika ziara hiyo amebaini mambo kadhaa yaliyopelekea shule hiyo kushika mkia.
Akitaja sababu alizozibaini alisema ni uchache wa walimu, ukosefu wa ukuta na kusababisha wahuni kuingia hovyo eneo la shule, wanafunzi kutoroka ovyo na mengineyo.
Diwani Obama alitaja sababu zingine alizozibaini ni mazingira mabaya ya shule hiyo kama vile wanawake na wanaume kuchangia choo kimoja.
Baada ya ziara hiyo diwani huyo alizunguuka mazingira ya shule hiyo na kujionea viti vingi na meza za kusomea vikiwa vimeharibika na kuwafanya wanafunzi wasome wakiwa wamekaa chini.
Alifika mpaka kwenye vyoo ambapo alishuhudia choo kimoja kikiwa hakitumiki baada ya kuharibika na kuhatarisha usalama na hivyo wanawake na wanaume kuchangia choo kimoja kilichobaki.
Akihitimisha ziara hiyo diwani Obama aliwaambia waliokusanyika kwenye ziara hiyo kuwa baadhi ya kero alizozifahamu kabla ya ziara hiyo alishazipeleka kwa maofisa wa wilaya hiyo ambao wamemuahidi ushirikiano katika kuboresha maendeleo ya shule hiyo.
Akihitimisha ziara yake aliwaahidi kushirikina na walimu na kamati ya maendeleo ya shule hiyo kuhakikisha shile hiyo inashika nafasi za juu.
“Niwaombe wazazi, walimu, viongozi wa kamati ya maendeleo wote tuwe kitu kimoja kuhakikisha tunapigania maendeleo ya shule yetu.
“Mimi binafsi ntafanya kila niwezalo kuhakikisha shule hii badala ya kuwa tena ya mwisho sasa inakuwa yakwanza” alisema diwani Obama huku akishangiliwa na wazazi ambao awali walionekana kukatishwa tamaa na watoto zao kusoma kwenye shule hiyo.
Naye Kaimu Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Lazaro Kulegea amemshukuru diwani huyo kufanya ziara hiyo shuleni hapo na kuchukua kero zao na kuahidi kuzifanyia kazi.
“Namshukuru sana mheshimiwa diwani kwa ziara yake hii na kuchukua changamoto alizozikuta kwa ajili ya kuzifanyia kazi jambo ambalo linaweza kuinusuru shule yetu na haya yaliyotokea kwenye matokeo yaliyopita.
“Nami niwasisitize tena walimu wenzangu, wazazi na kamati ya maendeleo kuzidi kuipambania shule yetu ili tuwe wakwanza badala ya kushika mkia kama ilivyokuwa matokeo yaliyopita” alimaliza kusema mwalimu mkuu.
HABARI/PICHA: RICHARD BUKOS /GPL