The House of Favourite Newspapers

Dkt. Mpango Asisitiza Kuchukua Tahadhari ya Corona

0

MAKAMU wa Rais  wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  Dkt. Philip Isdor Mpango  Juni 27, amefungua Mkutano Mkuu wa Baraza la Waislamu Tanzania (BAKWATA) ambao umefanyika Jijini Tanga.

 

Makamu wa Rais amewaomba viongozi wa dini kuendelea kuliombea taifa, kuwahimiza wananchi kufanya kazi ambazo ni halali, kudumisha amani na umoja katika taifa, kusisitiza maadili mema kwa jamii pamoja na umuhimu wa kuhifadhi mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabia ya nchi.

 

Aidha, Dkt. Mpango amewasihi viongozi wa dini kuendelea kuwahimiza waumini kuchukua tahadhari juu ya janga la corona, ikiwa ni pamoja na kufuata maelekezo yote yanayotolewa na wataalamu wa afya nchini.

 

Makamu wa Rais amesihi BAKWATA, Viongozi wote wa dini ya Kiislamu na dini nyingine na pia Wakuu wa Taasisi zote za Dini kujitahidi kuziendesha Taasisi hizo kwa mujibu wa Katiba zao na mafundisho ya dini.

 

Awali akisoma hotuba ya BAKWATA Katibu wa Baraza hilo Sheikh Nuhu Jabir Mruma amesema Bakwata itaendelea kushirikiana na serikali pamoja na kuwahimiza waumini wa dini ya Kiislamu kulipa kodi kwa manufaa ya taifa.

 

Kwa upande wake Mufti Mkuu wa Tanzania Aboubakar Zuber Bin Ali amewataka Waislamu nchini kote kuongeza umoja na mshikamano ambao utaleta utulivu katika nchi.

Leave A Reply