JK Awapasha Wana-Yanga
RAIS mstaafu wa Tanzania wa awamu ya nne Jakaya Mrisho Kikwete Juni 27, alikuwa mgeni rasmi katika mkutano mkuu wa Yanga kupitisha rasimu ya mabadiliko ya uendeshaji wa klabu hiyo aligeuka kivutio kwa hotuba na simulizi zake zilizojaa mzaha na masikhara.
Kikwete aligeuka kivutio kikubwa kwenye hotuba yake pamoja na kuikumbusha klabu yake pendwa maarufu kama ‘wananchi’ kufanya usajili mzuri kwa wachezaji wenye hadhi pamoja na kuvumilia makocha, lakini hakuacha kuchomekea imani za kishirikina katika timu hiyo miaka ya nyuma.
“wachezaji hawawezi kuja leo mnataka ubingwa, yaani kocha anakuja leo, katikati ya msimu mwingine, mwisho wa msimu mwingine halafu mnataka mabadikiko. Lazima tuwe na subra.”
“Hakikisheni makocha na wachezaji wanahudumiwa vizuri, wasiwe wanadai mishahara ya mechi mbili au tatu halafu ukiwapeleka kwenye mechi ngumu wakashindwa unasema wamekuhujumu, sasa wamekuhujumu vipi hujamlipa mishahara?
Mkutano huo uliofanyika katika ukumbi wa DYCC uliyopo Temeke na kufungiliwa rasmi saa 4:00 asubuhi ,ulikuwa na ajenda kadhaa zinazolenga kuijenga upya klabu, japo ile yenye nguvu ilikuwa kubariki mchakato wa mabadiliko ya klabu kwenda kwenye mfumo wa uwekezaji.
Pia wajumbe wa mkutano mkuu walionekana kufurahishwa zaidi na uwakilishwaji wa mpango wa ujenzi wa makazi ya wachezaji na viwanja vya kuchezea kule Kigamboni.