The House of Favourite Newspapers

Gomes Amuanika Mganga wa Manula Simba

0

KOCHA Mkuu wa Simba Mfaransa Didier Gomes ametaja siri ya kiwango cha kipa wake namba moja Aishi Manula kuongezeka hivi sasa akiwa na timu ya taifa, Taifa Stars na klabu yake.

 

Hiyo ni baada ya kuzua mijadala katika mitandao ya kijamii kutokana na kiwango hicho pamoja na kumwagiwa sifa na Shirikisho la Soka Afrika (Caf) kupitia mitandao yake ya kijamii.

 

Manula ameweka rekodi ya kutoruhusu bao katika hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika akiwa amecheza michezo mitatu kati ya minne ya makundi dhidi ya AS Vita, Al Ahly na Al Merreikh.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Gomes alisema kocha wake mpya wa makipa Mbrazili Milton Nienov ndiye aliyemuongezea ubora wa kuokoa michomo golini kwake.

 

Gomes alisema kuwa tangu kocha huyo amejiunga na timu hiyo ameonekana akiwapa mbinu tofauti za kuokoa hatari golini, ambazo leo hii zinamfanya Manula na makipa wenzake Beno Kakolanya na Ally Salum kuonekana bora.

Aliongeza kuwa kitu kingine alichoongezewa kipa huyo ni hali ya kujiamini akiwa golini kwake na hiyo imemfanya ubora wake uongezeke zaidi.

 

“Manula ni kati ya makipa bora niliowahi kukutana nao katika baadhi ya timu nilizopita kuzifundisha, hivyo nina imani naye sana akiwepo golini.

“Wengi wamekuwa wakihoji ubora wake kuongezeka, ukweli ni kwamba kocha mpya wa makipa aliyejiunga na timu Milton ndiye anayefanya yeye aonekane bora katika kila mchezo.

“Kwani amekuwa akimpa mbinu mbalimbali zitakazomuwezesha kuokoa hatari golini kwake.

Pia amemuongezea hali ya kujiamini awapo golini kwake yeye pamoja na wenzake Kakolanya na Ally,” alisema Gomes.

STORI: WILBERT MOLANDI, DAR ES SALAAM

 

Leave A Reply