The House of Favourite Newspapers

Gomes Awaandalia Wabotswana Dozi Nzito

0

KOCHA Mkuu wa Simba, Didier Gomes, ameamua kuwaandalia dozi nzito wapinzani wake, Jwaneng Galaxy ambao wikiendi hii watakwenda kupambana katika mchezo wa kwanza wa Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya kwanza.

Simba inaanzia ugenini katika hatua hiyo, kabla ya marudiano Oktoba 24, Dar es Salaam ambapo mshindi wa jumla anafuzu hatua ya makundi.

Kuelekea mchezo huo, Gomes amesema hawawezi kuwadharau wapinzani wao, bali wanachokifanya ni kuiandaa timu kupata ushindi wa uhakika ugenini, kisha kumaliza kazi nyumbani, huku lengo likiwa ni kufuzu hatua ya makundi.

Akizungumza na Spoti Xtra, Gomes alisema: “Kila mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika ni mgumu, haijalishi unacheza na mpinzani wa aina gani, hilo ni jambo muhimu na tunalitambua vizuri.

“Wakati tunaenda kucheza dhidi ya Jwaneng Galaxy, maandalizi tunayoyafanya si ya kubeza bali tunafanya maandalizi kama ambavyo tulivyokuwa tukijiandaa dhidi ya timu ngumu tulizokutana nazo msimu uliopita wakiwemo Al Ahly, kwa dhumuni la kuhakikisha tunasonga mbele na kufuzu hatua ya makundi.”

Ikumbukwe kuwa, msimu uliopita, Simba iliishia robo fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kuondoshwa na Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini kwa jumla ya mabao 4-3. Ugenini ilifungwa 4-0, nyumbani ikashinda 3-0.

Mbali na mchezo huo ulioonekana mgumu, pia Simba ikiwa nyumbani, ilizifunga Al Ahly, AS Vita na Al Merrikh katika hatua ya makundi.

~~LUNYAMADZO MLYUKA, Dar es Salaam

Leave A Reply