Katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kuokoa maisha ya wagonjwa wanahitaji damu, kampuni ya simu ya Halotel leo tarehe 6, Machi, 2023 imeshirikiana na imeungana Shule ya Sekondari ya Wasichana na Taasisi ya Mifupa (MOI) kuandaa tukio kubwa la uchangiaji damu kwa hiari.
Zoezi hili litawajumuisha wadau kutoka taasisi mbalimbali za shule kutoka mkoani Dar Salaam.
Kuelekea Siku ya Wanawake Duniani mnamo tarehe 8 Machi ya kila mwaka, Halotel imeina ni muhimu kusherehekea siku hiyo kwa kuchangia katika sekta ya afya katika kuunga mkono juhudi za Serikali kuboresha sekta hiyo kwa maendeleo ya nchi.
Halotel kwa kushirikiana na MOI imewezesha utekelezaji wa kampeni ya uchangiaji damu chini ya shule ya sekondari Kisutu kwa kuchangia vifaa mbalimbali ikiwemo Tisheti, chakula, vinywaji na vitafunwa kwa ajili ya kutumika wakati wa zoezi la uchangiaji damu litakalofanyika siku ya tarehe 06/03/2023 katika viwanja vya shule ya sekondari Kisutu jijini Dar Es Salaam.
Akiongea katika tukio la kukabidhi vifaa hivyo, Mkuu wa kitengo cha masoko Halotel, Bi Sakina Makabu amesema: ” Hii ni katika kuhakikisha kwamba tunaipunguzia Serikali ya Awamu ya Sita mzigo katika kupunguza changamoto ya kukosekana kwa damu ya kutosha kuokoa maisha ya wagonjwa katika taaisisi ya MOI na hospitali ya Muhimbili.”
Aliongeza: “Wajawazito, manusura wa ajali, watoto chini ya miaka mitano wapo katika kundi lenye uhitaji mkubwa wa damu, hivyo kuwezesha zoezi hili ni ishara ya upendo wa kampuni kwa Watanzania ambao pia ni wateja wake.”
Zoezi hilo linatarajiwa kushirikisha zaidi ya shule 40 ambazo zitaleta wanafunzi zaidi ya 2000. Kwa upande wake, Afisa Habari wa MOI, Patrick Mvungi, taasisi imefurahishwa kwa mwitikio kutoka kampuni ya Halotel kwa kuwezesha kampeni ya Shule ya Sekondari Kisutu ya uchangiaji damu.
“Hii inaonesha namna kampuni inavyojali afya za wananchi na juhudi zinazofanywa na Serikali katika kuboresha sekta ya afya. Hii ni hatua kubwa kwetu kuelekea kuimarisha zaidi uhusiano wetu na kampuni ya Halotel katika kuboresha sekta ya afya,” Bw Mvungi amesema.
Kwa upande wake, Mkuu wa Shule ya Sekondari Kisutu, Bi Chiku Mhando, ameishukuru Halotel kwa kuwa mdhamini wa tukio hilo muhimu, na akawaomba watu binafsi, makampuni na taasisi mbalimbali kujitokeza kuunga mkono zoezi hilo ili kuongeza kiwango cha damu kwenye benki ya damu.
Sera ya Kampuni ya Halotel siyo tu imejikita kibiashara bali pia ni kusaidia jamii, kurudisha sehemu ya faida kwa jamii ili kusaidia Serikali za kuboresha sekta ya afya na elimu.