Wilbert Molandi | CHAMPUIONI|Dar es Salaam
MWENYEKITI wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe ametamka kuwa kuondoka kwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Yanga, Yusuf Manji kutawapa nafuu wao.
Kauli hiyo ameitoa ikiwa ni siku chache tangu Manji atangaze kuondoka kuiongoza Yanga kwa kile alichodai kuwapisha wengine kuiongoza timu hiyo inayojiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu Bara na Ligi ya Mabingwa Afrika.
Manji tangu ameingia kuiongoza Yanga akiwa kama mwenyekiti wa timu hiyo mwaka 2012, ameipa mafanikio makubwa ikiwemo kutwaa mataji matatu mfululizo ya ligi kuu, lakini pia Kombe la FA na Kombe la Kagame mara moja.
Akizungumza na Championi Ijumaa, Hans Poppe alisema kuwa Manji ndiye alikuwa kikwazo kwao kwenye mambo mbalimbali ikiwemo usajili wa wachezaji kutokana na udhamini mkubwa aliokuwa anautoa kwenye klabu hiyo.
Hans Poppe amesema mwenyekiti huyo alikuwa anafanikisha kambi za nje ya nchi ikiwemo nchini Uturuki ambayo Simba ilikuwa ngumu kutokana na kukosa udhamini mzuri kama waliokuwa wanaupata Yanga.
“Kama unakumbuka wakati anaingia madarakani ni yeye aliyefanikisha kumtoa Kaseja (Juma) Simba tukiwa tunamhitaji kwa kumsajili kwa dau la shilingi milioni 50.
“Kingine ni uwezo wake wa kifedha wa kwenda kuiweka timu kambi nje ya nchi ikiwemo Uturuki wakati sisi tukiwa hapa nchini, hivyo Yanga watamkumbuka sana.
“Na Yanga watamkumbuka kwa kushindwa kutumia fedha zake za udhamini vizuri, ninaamini kama Yanga wangezitumia vema fedha zake, basi naamini wasingekuwa tegemeo na wangejiendesha wenyewe,” alisema Hans Poppe na kuongeza:
“Wao walizoea kula katika hoteli za kitalii lakini sasa hivi hawawezi kupata mambo kama hayo, si unaona hata walipokuwa Mwanza katika mchezo wao wa mwisho wa Ligi Kuu, uliona hoteli waliyofikia, picha walizopiga wakisherehekea ubingwa zilionyesha siyo hoteli kama ambavyo walizoea kufikia wakati wa Manji.
Wakati wa utawala wa Manji, alifanikiwa kuwasajili Kelvin Yondani kutoka Simba, Mbuyu Twite aliyekuwa akiwaniwa na Simba na tayari alikuwa amekamilisha baadhi ya makubaliano na Simba.
GLOBAL TV Online, Kupitia kipindi chake cha Michezo, SPOTI HAUSI, kinazungumza EXCLUSIVELY na Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili wa Timu ya Soka ya Simba Sport Club, Zacharia Hans Poppe ambaye anafunguka mengi kuangazia klabu yake na soka la bongo kwa ujumla.