Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe.
Ibrahim Mussa, Dar es Salaam
MWENYEKITI wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe, ametamka wazi kuwa wachezaji wote wanaoweka fedha mbele na wasiokuwa na mapenzi na timu hiyo hawatakuwa nao msimu ujao.
Hans Poppe ameyasema hayo baada ya hivi karibuni baadhi ya wachezaji wa Simba kugoma kwenda Songea kucheza mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Majimaji wakishinikiza kulipwa mishahara yao.
Wachezaji wa timu ya Simba.
Wachezaji waliogoma ni wale wa kigeni ambao ni Hamisi Kiiza, Juuko Murshid, Emery Nimubona, Justice Majabvi, Vincent Angban, Brian Majwega na Paul Kiongera, lakini baadaye Majabvi na Angban waliungana na timu.
Hans Poppe amesema: “Hatutaendelea kuwa na wachezaji wasiokuwa na mapenzi na timu, haiwezekani mshahara uchelewe kidogo halafu unagoma, mbona hata serikalini mishahara inachelewa na watu wanafanya kazi.
“Hii haipo Simba tu, wanapaswa kutambua kwamba wapo kwa ajili ya kuipigania timu na masuala hayo yakitokea si sisi bali mazingira ndiyo husababisha, bora tubaki na wachezaji wenye mapenzi na timu.”
Kauli hiyo ya Hans Poppe inamaanisha kuwa, Kiiza na Juuko wana nafasi ndogo ya kubaki Simba kwani huwa hawataki kucheleweshewa mishahara yao.