The House of Favourite Newspapers

Hivi Ndivyo Dawa Mpya Inavyozuia Ukimwi

 

DAR ES SALAAM: Wengi hawajui hii dawa-kinga inayoanza kutolewa na Serikali kuzuia maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi (VVU) inafanyajefanyaje kazi, ndiyo kisa cha Uwazi kuleta habari hii ili kuwaelimisha wananchi.

Taarifa njema iliyotolewa hivi karibuni na Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ilisema kuwa, kimegunduliwa kidonge aina ya PrEP ambacho mtu akikitumia atajikinga na maambuzi ya Ugonjwa wa Ukimwi.

 

HALI ILIVYO MITAANI

Tangu uwepo wa mpango wa kuwapatia wananchi dawa-tiba hiyo ya Ukimwi, hali ya mambo mitaani iligeuka kwa wananchi wengi kusherehekea wakiamini kuwa muda wa kuweka chini silaha za kinga umewadia.

Uwazi, katika pitapita yake sehemu mbalimbali na hasa mijini lilibaini kuwa makundi ya vijana, machangudoa na wale wanaopenda ‘kucheza peku’ ndiyo waliofurahia upatikanaji wa dawa-kinga hiyo. “Kama Tanzania imefikia hapa, basi tumeendelea, nilivyokuwa sipendi kutumia kondomu mimi ningependa niwe kwa kwanza kupewa kinga hiyo,” alisema Frank Charles, mkazi wa Masaki jijini Dar.

 

PrEP NI NINI?

Dawa hii ambayo wizara ya afya imepewa kibali na Taasisi ya Taifa ya Magonjwa ya Binadamu (NIMRI) kuifanyia utafiti hapa nchini kuanzia mwaka huu, iligunduliwa kwa mara ya kwanza mwaka 2012 nchini Marekani ambako ilipata mafanikio makubwa.

PrEP ni kidonge kinachotokana na maneno ya kitaalam ya Pre- Exposure Prophylaxis ambacho kazi yake ni kuzuia maambukizi ya Ukimwi kutoka kwa mgonjwa kwenda kwa mtu mwingine.

 

VVU NI NINI?

Kabla ya kuichambua kwa ndani zaidi PrEP, ni muhimu kufahamu VVU ni nini na jinsi gani hufanya kazi. VVU ni virusi ambavyo kama virusi vingine haviwezi kujizalisha vyenyewe ambapo ni lazima vijichimbie na kuidhuru seli inayoishi ili virusi hivyo viweze kukua na kuenea.

VVU hushambulia moja kwa moja mfumo wa mwili kujikinga na magonjwa, hususan seli nyeupe za damu zinazojulikana kama CD4 ambazo hujulikana pia kama seli-T au seli zenye kutoa msaada. Seli hizo hufanya jukumu kubwa katika mfumo wa mwili kujikinga dhidi ya magonjwa.

 

PrEP INAVYOMLINDA MTU

PrEP ni dawa iliyotengenezwa maalum kwa watu wasiokuwa na maambukizi ya VVU, lakini wakiwa katika mazingira hatari ya kuambukizwa. Dawa hiyo ni kidonge ambacho ni lazima kimezwe kila siku kulingana na maelekezo ya daktari ili kuweza kupata matokeo mazuri zaidi kwa mtumiaji.

Ilielezwa kwamba, kidonge hicho ambacho kimejipatia umaarufu mkubwa nchini Marekani kwa kusaidia kupunguza maambukizi ya Ukimwi kimetengenezwa kwa kujumuisha dawa ya aina mbili, ya emtricitabine na tenofivir na kimekuwa kikiuzwa chini ya jina la Truvada.

Uchunguzi umeonesha kwamba, ikitumika inavyotakiwa, PrEP ina uwezo wa kupunguza hatari ya kuambukizwa VVU kwa njia ya ngono kwa zaidi ya asilimia 90 na humkinga mtu dhidi ya maambukizi hayo kwa uchangiaji wa kujichoma sindano za madawa ya kulevya kwa zaidi ya asilimia 70.

 

INAFANYAJE KAZI?

Dawa hiyo hufanya kazi moja kwa moja kwa kuzilinda CD4 dhidi ya kuingiliwa na VVU na kuzaliana. Hii inamaanisha kwamba hata kama VVU vitaingia mwilini mwa mtu, vitakuwa havina njia yoyote ya kudhuru mfumo wa kinga ya mwili. Isitoshe, VVU haviwezi kuzaliana bila ya CD4, hivyo kuvifanya virusi hivyo visienee.

Ifahamike kwamba, dawa hii haifanyi kazi kwa mara moja hivyo ni lazima mtu ameze kidonge hicho mfululizo sawa na maelekezo ya daktari kwa idadi ya vidonge atakavyokuwa amepangiwa kumeza kwa siku husika.

 

JE, PrEP NI SALAMA?

Kwa jumla, Mamlaka ya Chakula na Dawa ya Marekani (CDC), nchi ambayo imekuwa ikiitumia dawa hiyo kwa muda mrefu inadai kwamba, bado haijajulikana kama panaweza kuwepo madhara makubwa au tishio kwa maisha kutokana na dawa hiyo.

Uchunguzi uliofanywa ni kwamba, dawa hiyo inaweza kusababisha madhara madogo kama vile kichefuchefu, kuumwa kichwa na kuharisha, lakini vyote hivyo vimeonesha kutochukua muda mrefu.

Vilevile, uchunguzi umeonesha kwamba kwa watu ambao hawajaambukizwa VVU, dawa hiyo haina madhara ya muda mrefu, ikiwa ni pamoja na wale ambao wameitumia hadi kufikia miaka mitano.

 

LAZIMA KUITUMIA PrEP?

PrEP ni kwa watu ambao hawajaambukizwa VVU, lakini wakiwa katika mazingira ya hatari ya kuambukizwa kupitia ngono au matumizi ya sindano na ndiyo maana mamlaka imependekeza kwa watu ambao wanaendeleza uhusiano wa ngono na wenza ambao tayari wameambukizwa.

Wengine ambao ni muhimu kwao kutumia dawa hiyo ni wale wanaofanya kazi haramu ya ukahaba na wamekuwa hawatumii kinga kufanya ngono huku wanaougua magonjwa ya zinaa kama vile kaswende na gono nao wanashauriwa kutumia.

 

PrEP NI KINGA SAHIHI?

Pamoja na ukweli kwamba, dawa hiyo ni kinga iliyopata mafanikio, lakini baadhi ya wataalam wa afya akiwemo Naibu Waziri wa Afya, Dk Faustine Ndugulile alipoongea na Uwazi alishauri kuwa, watumiaji wa dawa-kinga hiyo hawatakiwi kuacha kutumia dawa nyingine au kondomu kwa lengo la kujihakikishia usalama zaidi.

Ni ukweli kwamba, dawa-tiba hiyo imetengenezwa maalum kwa ajili ya kinga dhidi ya Ukimwi na siyo magonjwa mengine ya zinaa hivyo ni vyema tahadhari ichukuliwe ili kuondoa uwezekanano wa kuambukizwa magonjwa mengine.

 

WAZIRI NA UWAZI

Mei 13, mwaka huu, Uwazi lilimtafuta Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Dk Faustine Ndugulile ili atolee ufafanuzi juu ya furaha waliyonayo wananchi juu ya upatikanaji wa dawa-kinga hiyo, ambapo alisema:

“Kwanza naomba ieleweke, kuna baadhi ya wananchi na hata vyombo vya habari vinapotosha ukweli na kusema kilichozinduliwa ni kinga, hii siyo kinga ni dawa-kinga.

“Kinachofanyika ni hivi; mfano mtu anaishi kwenye nchi ambayo haina ugonjwa wa malaria, akitaka kusafiri kwenye nchi yenye ugonjwa huo, atapatiwa dawa-kinga ili akienda huko asipate maambukizi.

 

“Na dawa-tiba tuliyoizindua itamuwezesha mtu ambaye hana maambukizi, lakini yuko katika hatari, atatakiwa kutumia dawa hiyo kwa lengo la kujikinga asiambukizwe pindi atakapofanya ngono bila kinga.”

Aliongeza kuwa, pamoja na kuanza kutolewa kwa dawa-kinga hiyo haitawahusu wananchi wote bali watapatiwa watu walio kwenye makundi maalum yanayotajwa kuwa yapo hatarini kuambukizwa Virusi vya Ukimwi (VVU).

Wasikie wadau wanasemaje na sheria inasemaje.

Mama Kanumba Afunguka Lulu Kuachiwa

Comments are closed.