The House of Favourite Newspapers

Hyperloop: Treni Inayoweza Kusafiri Kutoka Dar es Salaam Mpaka Kigoma Kwa Saa 1

0

Dunia inakwenda kwa kasi kubwa kuliko kawaida.

Wakati Tanzania ikiwa inapambania kombe kujenga reli ya SGR, wenzetu walishavuka huko kitambo.

Japan walianza kutumia treni za umeme mwaka 2010, ikafuatiwa na China. Treni zao zilikuwa na uwezo wa kusafiri kwa kasi ya kilometa 380 mpaka 480 kwa saa.

Lakini huo haukuwa mwisho wa uvumbuzi, wanasayansi wakaja na teknolojia ambayo mpaka sasa ndiyo inayoaminika kuwa ya kisasa zaidi, Maglev ambayo ni kifupi cha maneno ‘Magnetic Levitation’.

Kwenye teknolojia hii, treni inakuwa na uwezo wa kukimbia kilometa 603 kwa saa na ilianza kutumika rasmi April, 2015 nchini Japan.

Sasa unaambiwa hiyo yote cha mtoto! Elon Musk kwa mara nyingine, anaishangaza dunia!

Kampuni yake ya Space X kwa kushirikiana na Kampuni ya Tesla, zimekuja na teknolojia mpya na ya ajabu katika usafiri wa treni, iitwayo Hyperloop ambayo ina kasi ya mara mbili zaidi ya treni za sumaku, Maglev!
Katika teknolojia ya Hyperloop, treni husafiri katika bomba maalum (vacuum tunnel) ambalo linakuwa limefungwa pande zote na haliruhusu hewa kutoka au kuingia.

Ndani ya bomba hili, kunakuwa na hewa iliyoongezwa pressure (compressed air) ambayo hufanya kitu chochote kusogea kutoka sehemu moja kwenda nyingine, kwa kasi kubwa zaidi ya ile ya uvutano wa sumaku.

Sasa kinachofanyika ni kwamba, kunakuwa na ‘bearings’ maalum za kisasa ambazo ndiyo zinatumika kama reli, yaani treni hiyo ya kisasa inakaa juu ya hizo ‘bearings’, halafu mashine za kisasa za kuongezea hewa mgandamizo (air compressor) zinafungwa kwa nyuma na zinakuwa zinaisukuma treni kwenda mbele kwa kasi kubwa sana.

Pia kunakuwa na nguvu ya uvutano kutokea mbele (linear induction) ambayo inaivuta treni kwenda mbele kwa kasi ambayo haijapata kutokea, nyuma inasukumwa na mbele inavutwa kwa wakati mmoja!

Majaribio ya awali yameshafanyika na kuonesha mapinduzi makubwa ya kiteknolojia, ambapo treni ya kwanza ya aina hiyo, Hyperloop 1 iliyofanyiwa majaribio nchini Marekani, imeweka rekodi ambayo haijawahi kufikiwa katika historia ya usafiri wa nchi kavu, ya kasi ya kilometa 1200 kwa saa, yaani kutoka Dar es Salaam mpaka Kigoma, ‘unateleza’ kwa muda wa saa moja tu, umeshafika.

@hashpower7113

Leave A Reply