The House of Favourite Newspapers

Ingizo Jipya Yanga SC Lakingiwa Kifua

0

FISTON Abdol Razack ingizo jipya ndani ya kikosi cha Yanga, amekingiwa kifua na Kocha Mkuu wa timu hiyo Cedric Kaze kwa kushindwa kuonyesha makeke ndani ya uwanja.

 

Nyota huyo ambaye amesaini dili la miezi sita, mchezo wake wa kwanza ilikuwa ni dhidi ya African Sports, Uwanja wa Azam Complex alitumia dakika 78 katika mchezo wa kirafiki na mchezo wake wa kwanza ndani ya Ligi Kuu Bara ilikuwa dhidi ya Mbeya City, Uwanja wa Sokoine.

 

Kwenye mchezo huo wakati Mbeya ikipata sare ya kufungana bao 1-1, nyota huyo alitumia dakika 74 na nafasi yake ilichukuliwa na Ditram Nchimbi, alishindwa kuonyesha makeke ambayo mashabiki wa Yanga walikuwa wanatarajia.

Kaze alisema kuwa bado hajajenga mazoea mazuri na wachezaji wenzake ndani ya uwanja hivyo atakuwa kwenye ubora wake kwenye mechi zake zijazo, mashabiki wasiwe na mashaka.

 

“Ni mchezaji mpya kwa sasa bado hajazoea ile mikimbio ya wachezaji wenzake kama ambayo naye hajawazoea, ila nina imani kwamba baada ya muda atakuwa kwenye ubora na atafanya vizuri ndani ya uwanja,” alisema.Leo Februari 17, Yanga ina kazi ya kusaka pointi tatu mbele ya Kagera Sugar inayonolewa na Mecky Maxime Uwanja wa Mkapa na kwenye mchezo wa kwanza msimu huu, Yanga ilishinda bao 1-0, Uwanja wa Kaitaba.

Leave A Reply