The House of Favourite Newspapers

Injinia Hersi Afuata Beki Mali

0

YANGAimeamua na safari hii haina utani kabisa katika usajili wa wachezaji hasa wa kimataifa kwa ajili ya maandalizi ya msimu ujao ambapo timu hiyo inatarajiwa kushiriki michuano ya kimataifa.Tayari Yanga kupitia kwa Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili, Injinia Hersi Said, imekamilisha usajili wa beki wa kulia raia wa DR Congo, Djuma Shabani aliyekuwa AS Vita.

 

Baada ya kukamilisha usajili huo, Injinia Hersi amekuwa na ziara kwenye nchi tofauti barani Afrika ikiwemo Afrika Kusini ambapo kwa sasa amerejea nchini huku safari yake ijayo ikitajwa ni Mali anapoenda kumchukua beki mahiri wa kati atakayekuja kuchukua mikoba ya Lamine Moro aliyeomba kuondoka.

 

Chanzo cha uhakika kutoka ndani ya Yanga, kimeliambia Spoti Xtra kuwa, Injinia katika safari yake ya kwanza alifanikiwa kukamilisha usajili wa wachezaji kadhaa ambao imekuwa ni siri kubwa na hakutaka taarifa zake zivuje licha ya kufahamika wachezaji aliofanya nao mazungumzo.

“Ilikuwa rahisi sana kuifahamu safari ya kwanza ya usajili wa Djuma Shabani ambapo Injinia Hersi alifanikiwa kukamilisha usajili wake na kiungo mshambuliaji, Mercey Vumbi Ngimbi naye wa DR Congo, lakini wachezaji wengine imekuwa ngumu kina nani amemalizana nao au bado wapo kwenye mazungumzo.

 

“Sasa baada ya Injinia kurejea, anatarajiwa kuondoka kwa ajili ya kwenda kukamilisha usajili wa wachezaji wengine wa kimataifa ambapo kuna mmoja kutoka Mali ambaye ni beki wa kati, huyo atakuwepo katika orodha ya safari ya pili,” kilisema chanzo hicho.

 

Mwenyekiti wa Kamati ya Ufundi ya Yanga, Dominick Albinus, alithibitisha timu hiyo kumsajili beki wa kulia wa AS Vita, Djuma Shabani, huku akiweka wazi kuwa mchezaji huyo anatarajiwa kuwasili hapa nchini hivi karibuni.

 

Mbali na Djuma, inatajwa kwamba Yanga imemalizana na Dickson Ambundo wa Dodoma Jiji na David Bryson wa KMC.Mjumbe wa Kamati ya Ufundi wa Yanga, Arafati Haji, amesema: “Yanga katika usajili wa kimataifa msimu huu tutafanya wa wachezaji wasiopungua na kuzidi watano, hiyo ni katika kuhakikisha tunafanya vizuri katika michuano ya kimataifa.”

MARCO MZUMBE, Dar es Salaam

RONZE Baada ya KUACHANA na SHILOLE Afunguka – “HANISAPOTI, ZUCHU na IBRAAH, MIMI MKUBWA Kuliko WAO”

Leave A Reply