The House of Favourite Newspapers

Ishu ya Nabi Kupewa Mechi Mbili tu, Yanga Yatoa Tamko Zito

0

UONGOZI wa Yanga umelifungukia sakata la kocha wao Mtunisia, Nasreddine Nabi juu ya kupewa michezo miwili. Hivi karibuni kulizuka tetesi za Nabi kupewa michezo miwili kushinda dhidi ya Rivers United watakaocheza nao Jumapili hii katika Ligi ya Mabingwa Afrika na ule wa Ngao ya Jamii watakaocheza na Simba.

 

Tetesi zilianza baada ya kupoteza mchezo uliopita dhidi ya Rivers kwa kufungwa bao 1-0 kwenye Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

 

Kwa mujibu wa Mjumbe wa Kamati ya Ufundi ya Yanga, Dominic Albinius, hizo ni taarifa za uongo na uzushi zenye lengo la kuwavuruga wakiwa katika maandalizi ya mchezo wao dhidi ya Rivers.

 

“Kumezuka taarifa za uongozi wa Yanga kumpa kocha Nabi mechi mbili zinazofuata kama hatma ya kibarua chake. Huu ni uzushi wa hali ya juu.

 

“Uongozi una imani kubwa kwa kocha Nabi na una mipango naye ya muda mrefu sana kwa maendeleo na mipango ya muda mrefu katika kukifanya kikosi cha Yanga kuwa tishio Afrika.

 

“Hizi ni propaganda za maadui zetu na wasiotutakia mema. Niwahakikishie kuwa kocha Nabi yupo sana katika kikosi chetu cha Wananchi.

 

“Kocha Nabi ni miongoni mwa makocha wachache Afrika wenye elimu ya juu sana katika ufundishaji wa soka na hili linadhirishwa na mafanikio aliyoyapata alipokuwa anafundisha klabu mbalimbali katika Afrika.

 

“Huu ni wakati ambao wananchi wote tunapaswa kushikamana na kuonyesha ukomavu wetu katika soka nchini. Sisi ni Wananchi na daima hatujawahi kukata tamaa.

 

“Kikosi kipo katika mikono salama ya makocha wetu, viongozi pamoja na wadhamini wetu na kamwe haturudi nyuma,” alisema Albinus.

 

WILBERT MOLANDI, Dar es Salaam

 

Leave A Reply