The House of Favourite Newspapers

Jambazi aliyetoroka kwa helikopta miezi 3 iliyopita akamatwa

Image result for Redoine Faid

Redoine Faid, jambazi sugu,  raia wa Ufaransa ambaye alitoroka jela akitumia helikopta iliyokuwa imetekwa nyara,  amekamatwa tena na polisi.

Mhalifu huyo aliyekuwa akisakwa na vyombo vya ulinzi nchini Ufaransa, alishikwa kaskazini mwa jiji la Paris, akiwa na ndugu yake na watu wengine wawili,  kwa mujibu wa ripoti ya polisi.

Faid, 46, amenukuliwa awali akisema kuwa yeye ni shabiki wa filamu za uhalifu, ambazo anadai zimemfundisha jinsi ya kufanya uvamizi. Mwaka 1998 alikamatwa kwa mara ya kwanza kwa shitaka la wizi wa kutumia nguvu.

Tukio la kutoroka jela mwezi wa Julai mwaka huu ni la pili kwa mhalifu huyo. Alitoroshwa kutoka gereza moja huko Reau, kusini-mashariki mwa Paris, na watu watatu waliokuwa na silaha kisha wakamuingiza kwenye ndege aina ya helikopta iliyoendeshwa na rubani aliyekuwa ametekwa nyara.

Image result for Redoine Faid

 

Kukamatwa kwake kunakuja saa kadhaa baada ya Waziri wa Mambo ya Ndani wa Ufaransa, Gérard Collomb,  kujiuzulu katika pigo jipya kwa  Rais Emmanuel Macron. Wizara hiyo itaongozwa kwa muda na Waziri Mkuu, Édouard Philippe.

Jambazi huyo anadai kuwa filamu za Hollywood, kama  filamu maarufu ya uhalifu ya Scarface iliyoigizwa na nyota Al Pacino, ilichangia mfumo wa maisha yake.  Wakati mmoja alienda kwa mtengeneza filamu hiyo, Michael Mann, kwenye tamasha ya filamu la Paris na kamwambia: “Wewe ulikuwa mshauri wangu wa kiufundi.”

Mwaka 2013 alitoroka jela mara tu baada ya kuwasili akitumia vilipuzi alipolipua milango mitano ya gereza huku akiwashika mateka walinzi na kuwatumia kama ngao.   Umaarufu wake umechangiwa na kitabu chake cha mwaka 2009, kinachosimulia maisha yake toka akiwa mdogo kwenye mitaa ya Paris mpaka kuwa mhalifu sugu.

Image result for Redoine Faid

Maisha ya Redoine Faid

  • Maisha ya Faid ya kufungwa jela na kutoroka yalianza mwaka 1998 kutokana na makosa ya wizi wa kutumia nguvu na kupora benki.
  • Mwaka 2009 aliachiliwa kwa msamaha akiapa kuwa alikuwa amebadilika lakini mwaka 2011 alikuwa amekiuka makubaliano ya kuachiliwa kwake na akarudishwa kifungoni.
  • Mwaka 2017 alihukumiwa miaka 10 jela baada ya kutoroka gereza la  Séquedin, mwaka 2013 nje ya mji wa Lille. Pia alihukumiwa miaka 18 kwa kupanga wizi mwaka 2010 ambapo polisi mmoja Aurélie Fouquet, aliuawa.
  • Faid alishindwa katika rufaa aliyoikata na Aprili mwaka 2018 alihukumiwa kifungo zaidi cha miaka 25 kwa wizi. Alikuwa akitumikia kifungo hicho wakati wa kisa cha hivi majuzi cha kutoroka jela
  • Alizaliwa mwaka 1972 na kukulia maeneo yenye visa vya uhalifu jijini Paris.
  • Miaka ya 1990 aliongoza genge lililohusika kwenye wizi na kupora watu jijini Paris.
  • Mmoja wa wasimamizi wa Faid gerezani alisema – “Hakuwa na mzozo wowote na walinzi lakini tulikuwa na hofu kila wakati.”

Credit: bbcswahili

BREAKING: ACT waicharukia NECTA kufuta Matokeo Darasa la 7

Comments are closed.