The House of Favourite Newspapers

Jifunze Lugha Ya Kuugusa Moyo Wa Mpenzi Wako…. Soma Hapa

0

RAFIKI, ni IJUMAA nyingine murua ambayo Mwenyezi Mungu ametujaalia hivyo hatuna budi kumshukuru.

Moja kwa moja tuingie kwenye mada yetu ya leo. Fahamu tu kwamba, ni vyema na ni muhimu kwa kila aliyepo kwenye uhusiano, mapenzi au ndoa kufahamu kwamba zipo namna za kuwasiliana na kufahamiana baina ya wapenzi.

 

Kama mmoja anakosea kwa kujua au kutokujua anakuwa analeta misuguano yenye athari kwenye penzi husika.

Kila mmoja hana budi kuifahamu lugha mwenzake anayoitumia kulionyesha penzi au kumaanisha penzi ili aweze kuyafanya mambo kwa mlengo uleule wa mpenzi wako na yeye vilevile akufahamu na kufanya mambo kupitia lugha yako.

 

Hapa kila mmoja anakuwa anaugusa moyo wa mwenzake na kuiongeza furaha katika mahusiano.

Unaweza ukawa unafanya mambo mengi mema kwa mpenzi wako lakini anaangalia na kunyamaza akifahamu ndani yake kwamba ni wajibu wako kufanya vile.

 

Wapo baadhi ya watu wenye kiu na maneno ya kupongezwa, kushukuriwa au ya kuhamasisha. Kwa mfano, mwenzako amekusaidia kuanua nguo zako nje, akimaliza au unapogundua nguo zimetolewa na lilikuwa jukumu lako kuzitoa, usione ugumu wa kumwambia mpenzi asante kwa kunisaidia kuanua nguo.

 

Anaweza akaamua kumlisha mtoto wewe ukiwa unafanya mambo mengine, usichukulie kirahisi tu kwamba na yeye si mzazi lazima amlishe mtoto pia, hapana, mwambie mpenzi nakushukuru umenisaidia kumlisha mtoto na mimi nikaweza kufanya hiki na kile.

 

Akipendeza mwambie umependeza, nguo hiyo inakutoa vyema sana, akifanya kitu hata kama ni kidogo mpongeze na kumwambia unatambua mchango wake mzuri. Wako wenye kiu kubwa na maneno haya na kwao wasipoyasikia ni kama vile hawajapendwa kabisa na unaposema neno hili kwake unanyanyua kitu kikubwa sana ndani yake.

 

Ni vyema ukafahamu kama mpenzi wako ni mwenye lugha hii ya mapenzi basi usimnyime chakula cha nafsi yake. Mpongeze, mshukuru na kumwambia maneno yenye hamasa yatakayomshibisha.

 

Nadhani unakumbuka ule usemi unaosemwa mara nyingi kwamba; ‘matendo hukidhi haja maridhawa kuliko maneno’, wengine wanasema maneno matupu hayavunji mfupa.

 

Misemo hii yote inatuma ujumbe mmoja kwamba maneno matupu yakiongewa tu pasipo matendo basi hakuna tija. Wapo ambao matendo ndicho kitu pekee cha wao kuonesha penzi na hata wao kulitafsiri penzi kutoka kwa mtu mwingine pia.

 

Hapa namaanisha, kwa yeye kukuonesha anakupenda atakuwa tayari kukufanyia kitu au kukusaidia kitu na ili ajue kwamba unampenda na yeye anatamani kuona wewe ukimfanyia kitu au vitu, anataka kuona matendo siyo maneno tu.

Yamkini una juhudi sana za kumwambia mpenzi wako kuwa unampenda sana na unafurahi kuwa naye maishani, haya ni maneno mazuri na makubwa sana.

 

Kama yeye ni mmoja ya watu wenye lugha ya matendo ya kuhudumia itakuwia ngumu kumuonesha unampenda kwa sababu kwake yeye upendo au mapenzi hayaonyeshwi kwa maneno bali kwa kumsaidia kitu au vitu.

 

Yeye anatarajia akiosha vyombo umsaidie kufuta, akiandaa chakula umsaidie kuandaa meza, akimalizia kuvaa umsaidie kumwandaa mtoto ili muwahi na vitu vingine kama hivi.

 

Cha ajabu ni kwamba kwa mmoja kutokuona mapenzi yakioneshwa kwa lugha yake basi anahitimisha kwamba hapendwi. Sasa angalia jinsi watu wawili wanaoishi nyumba moja kama mtu na mkewe, kila mmoja akifahamu fika kwamba anampenda mwenzake lakini mmoja anaona kabisa kuwa hapendwi.

 

Lakini kama wakisaidiwa kuzifahamu lugha zao za penzi basi kila mmoja atamfahamu mwenzake na kuongea kwa lugha yake.

 

Katika jamii mbalimbali kwa miaka mingi sana kutoa zawadi kwa mtu au watu kumekuwa kukitazamwa kama ishara ya kuonesha upendo, na mtu mwenye tabia ya kutoa zawadi mara kwa mara basi anaonekana kwenye jamii husika kwamba ni mtu mwenye upendo sana. Kutoa zawadi ni kitu cha asili maana ndani ya kila nafsi ya mwanadamu kuna kitu kinachotuhamasisha kwamba kama ninampenda ni lazima niwe tayari kumpa kitu na kama ananipenda basi atakuwa tayari kunipa kitu.

 

Kila mtu anapenda kupokea zawadi, lakini wapo ambao kwao kutoa zawadi ndiyo lugha yao kuu ya kulionesha penzi lao kwa mtu na wao kupokea zawadi huhesabiwa ni alama kubwa ya kuonyeshwa upendo au mapenzi. Watu wa kundi hili wao kutoa au kupokea zawadi hakuna tu ile furaha ya kawaida bali kuna msisimko wa kitofauti sana na tafsiri ya zawadi ni kubwa zaidi kuliko kwa mtu mwingine. Anapotoa zawadi kweli anahisi amekupenda sana na unapompa zawadi kwa kweli anafurahi katika namna ya kukosa maelezo.

 

Kama umeoana na mtu wa namna hii, jitahidi sana kutokukaa muda mrefu bila kumletea vitu kama maua, mnunulie kitu anachokipenda, mnunulie ice cream, nunua kanguo kanakomtosha akakute kitandani, mpeleke sehemu mwambie chagua kitu unachokipenda.

 

Na hapa nisisitize kwamba zawadi haimaanishi kitu au vitu vya gharama maana tafsiri ya uthamani wa zawadi kwa watu hawa haiangaliwi kwa gharama iliyohusika bali moyo ulioiwaza zawadi hiyo. Usiache siku yake ya kuzaliwa ikapita haujampa chochote.

Kwa leo ninaishia hapa, tukutane IJUMAA ijayo. Kwa maoni na ushauri, wasiliana na mimi

Leave A Reply