Jike Shupa; Aishi Ghorofani Kumfurahisha Mumewe
Zena Abdallah ‘Jike Shupa’.
MAMBO vipi mpenzi msomaji wa Mpaka Home? Leo tunaye mwanadada Zena Abdallah ‘Jike Shupa’ ambaye ndiye video queen wa Wimbo wa Jike Shupa wa Mwanamuziki Naftal Mlawa ‘Nuh Mziwanda’ ambao umezaa jina lake.
Wimbo huo, Nuh amemtumia mrembo huyo kuakisi maadhui ya kumfananisha na mpenzi wake wa zamani, Zuwena Mohammed ‘Shilole’ waliyemwagana huku kila mmoja akimpa vijembe mwenzake.
Jike Shupa anaishi Kariakoo. Kujua mengi kuhusu mrembo huyu, twende pamoja:
Mpaka Home: Kwa nini umeamua kukaa huku ghorofani?
Jike Shupa: (Kicheko) Hapa ndiyo mtu wangu anaishi hivyo na mimi lazima nikae tu.
Mpaka Home: Kwani umeolewa?
Jike Shupa: Ndiyo.
Mpaka Home: Harusi yenu ilikuwaje?
Jike Shupa: Ha ha ha! Ilikuwa kimyakimya na sipendi hata kuizungumzia sana kwenye media.
Mpaka Home: Unapenda kufanya nini ukiwa nyumbani?
Jike Shupa: Kupika, kiukweli nina weza kushinda nikijipikilisha vitu vingi kwa siku utafikiri nina sherehe.
Mpaka Home: Sasa ukijipikilisha vitu vingi na nyinyi mpo wachache, inakuwaje?
Jike Shupa: Nawapigia marafiki zake mume wangu na watu wangu wa karibu wanakuja kujumuika, nami ndiyo furaha yangu.
Mpaka Home: Kipindi cha nyuma uliwahi kubeba ujauzito wa mwanamuziki mkubwa sana Bongo, Juma Nature vipi mtoto wenu yuko wapi sasa hivi?
Jike Shupa: Mtoto wangu mkubwa sasa ana miaka 10, anaitwa Naila na yuko nyumbani kwetu.
Mpaka Home: Kwani mna bifu yoyote na Shilole?
Jike Shupa: Hapana na huwezi amini kama ningejua kile nilichokuwa nimeimbiwa niigize kwenye ule wimbo kuwa nilikuwa namuigiza yeye (maisha ya Shilole na Nuh), nisingefanya ila sikujua kabisa.
Mpaka Home: Unapokuwa nyumbani muda wako mwingi unautumia kufanya nini?
Jike Shupa: Napenda sana kulala, muda mwingi nautumia kupumzika maana mambo ya kuzunguka jiji yalikuwa kipindi cha nyuma.
Mpaka Home: Nashukuru kwa ushirikiano wako.
Jike Shupa: Haya karibu tena.