RAIS John Magufuli leo Jumatatu, Agosti 24, 2020, amewasilisha fedha za michango iliyotolewa katika harambee ya kuchangia ujenzi wa msikiti wa Chamwino mkoani Dodoma.
Fedha hizo zimewasilishwa na Katibu wa Rais Bw. Ngusa Samike kwa Sheikh Mkuu wa Wilaya, Suleiman Abdallah Matitu, muda mfupi baada ya swala ya adhuhuri iliyofanyika katika msikiti uliopo hivi sasa.
Pamoja na kukabidhi fedha hizo, Magufuli amewapongeza na kuwashukuru watu wote waliounga mkono na wanaoendelea kuunga mkono uchangiaji wa ujenzi wa msikiti mpya na wa kisasa wa Wilaya ya Chamwino.
Amesema msikiti huo utajengwa na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) na ujenzi wake utaanza wiki hii. Amesema watu mbalimbali wameguswa bila kujali madhehebu ya dini waliyonayo na kwamba hiyo ni udhibitisho wa umoja na mshikamano walionao Watanzania.