The House of Favourite Newspapers

Kagere, Mugalu Hatihati Kuikosa Yanga

IMEELEZWA kuwa huenda washambuliaji hatari wa Simba, Meddie Kagere na Chris Mugalu, wakaikosa mechi dhidi ya Yanga kutokana na majeraha waliyoyapata hivi karibuni. Simba na Yanga zinatarajiwa kukutana kwa mara ya kwanza msimu huu, Novemba 7 kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar.

 

Kagere Kagere, Mugalu hatihati kuikosa Yanga anasumbuliwa na maumivu ya enka aliyoyapata katika mchezo wa JKT Tanzania Oktoba 4 ambao Simba walishinda 4-0, Mugalu yeye anasumbuliwa na misuli aliyoumia wakati wa maandalizi ya mechi dhidi ya Tanzania Prisons ambayo Simba walifungwa 1-0 Oktoba 22.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, juu ya wachezaji hao kocha mkuu wa Simba, Sven Vandenbroeck, alisema kuwa Kagere anahitaji muda wa wiki mbili hadi tatu ili kuanza kucheza huku akisema kuwa Mugalu pia hali yake haijakaa sawa tayari kwa kucheza.

 

“Kagere kwa sasa bado ni majeruhi na anahitaji wiki zisizopungua mbili mpaka tatu mpaka hali yake kukaa sawa, sina uhakika kama atapatikana kwenye mchezo dhidi ya Yanga.

 

“Kuhusu Mugalu pia bado hajaanza mazoezi na wenzake ninavyofahamu naye ni majeruhi lakini tunatarajia kupata ripoti ya madaktari hivi karibuni kuona kama atarejea uwanjani haraka,” alisema Mbelgiji huyo.

 

Kagere na Mugalu kwa pamoja kwenye michezo ya ligi kuu wameifungia Simba mabao saba ambapo Kagere amefunga manne huku Mugalu akifunga matatu.

Marco Mzumbe, Dar es Salaam

Comments are closed.