Kajala Azindua Kampeni Ya Taulo kwa Mabinti Shuleni – Video
KAMPUNI ya Gerirwa General Supplies ya jijini Dar ambayo pia ni wasambazaji wa taulo za kike za Rani, leo imezindua kampeni ya kijamii iitwayo Rani na Binti Shuleni ambayo inalenga kusaidia wanafunzi wasioweza kuhudhuria shuleni wawapo katika hedhi kwa kuwapa taulo za kike.
Shule zilizolengwa ni zile za sekondari ambazo zipo chini ya serikali za mikoa yote hapa nchini. Mpango huu unaenda sambamba na kampeni ya serikali ya kutoa elimu bure ili mtoto wa kike asibaki nyuma. Kupitia kampeni hiyo wakurugenzi wa Gerirwa, Hudaa Badi na Hawa Hassani, wamemtambulisha rasmi msanii wa Bongo Muvi, Kajala Masanja, kuwa balozi wa taulo hizo.
Wakurugenzi hao wamesema mwananchi yeyote anaweza kupendekeza shule yeyote ya sekondari ya serikali ambayo anaona wanafunzi wake wanahitaji msaada wa taulo hizo kutokana na hali yao kimaisha kwa kutuma ujumbe kwenye namba 0754 311 616 au kupitia akaunti ya Instagram #ranisanitarypad.
Katika hafla hiyo, Kajala amesema ana furaha kubwa kuwa sehemu ya mpango wa kuwasaidia mabinti hao wadogo ambao ni umri wa mwanaye, Paulo, ambaye naye anashiriki sehemu ya ubalozi wa mama yake.
Akizizungumzia taulo hizo Mkurugenzi wa Gerirwa, Hawa Hassani, amesema zimetengenezwa kwa ubora wa hali ya juu kwa kutumia teknolojia ya anion ambayo inatibu kadhia mbalimbali zinazosababishwa na hedhi ambapo bidhaa hizi zimethibitishwa na mamlaka ya madawa na vifaa tiba ya TMDA.
STORI: RICHARD BUKOS | GPL