The House of Favourite Newspapers

Kichuya Kuanza na Mwadui FC Kesho Taifa

0

KIKOSI cha Simba, kesho Jumamosi kitashuka uwanjani kupambana na Mwadui FC katika mchezo wa Kombe la FA utakaochezwa kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam.

 

Hata hivyo, wapenzi na mashabiki wa Simba wanaweza kumwona uwanjani Shiza Kichuya akiitumikia timu hiyo kwa mara ya kwanza baada ya kujiunga nayo hivi karibu akitokea nchini Misri katika Klabu ya Pharco inayoshiriki Ligi Daraja la Pili nchini Misri ambayo ilimsajili msimu uliopita akitokea Simba.

 

Katika dirisha dogo la usajili lililofungwa hivi karibuni, Simba ilimsajili Kichuya ambaye hapo awali alikuwa mmoja kati ya wachezaji wa kutumainiwa wa timu hiyo kwa ajili ya kuiongezea nguvu safu yake ya ushambuliaji.

Habari kutoka ndani ya Simba ambazo Champini Ijumaa limezipata zimedai kuwa, kwa mara ya kwanza Kichuya anaweza kuonekana katika mchezo huo.

 

“Kichuya ameanza jana (juzi) mazoezi na timu baada ya kusajiliwa hivi karibuni, hata hivyo katika mazoezi hayo alionyesha uwezo mkubwa na kumvutia kocha.

 

“Kwa hiyo kama mambo yatakuwa vizuri basi katika mchezo wa Jumamosi dhidi ya Mwadui anaweza kuitumikia timu yetu kwa mara ya kwanza,” kilisema chanzo hicho cha habari.

 

Hata hivyo, Kocha Mkuu wa Simba, Mbelgiji, Sven Vanderbroeck alipoulizwa alisema: “Ni mchezaji mzuri nimemuona mazoezini lakini siwezi kusema kama nitamtumia au sitamtumia katika mechi hiyo.”

Leave A Reply