The House of Favourite Newspapers

Kiwango cha Chama Kudaiwa Kuporomoka, Staa Simba Aanika Haya

0

LICHA ya baadhi ya mashabiki wa soka kuonyesha kutoridhishwa na kiwango cha kiungo, Cleotus Chama kwenye mchezo ambao Simba ilikubali kipigo cha bao 1-0 ugenini dhidi ya Kagera, kiungo fundi wa zamani wa Simba, Mtemi Ramadhan amekuwa tofauti na kiwango alichokionyesha Chama kwenye mchezo huo.

 

Chama ambaye amerejea Simba msimu huu wa usajili wa dirisha dogo baada ya kuuzwa na timu hiyo mwaka 2021, jana alikuwa miongoni mwa nyota waliochapwa kwenye uwanja wa Kaitaba mjini Kagera, Januari 26, 2022.

 

Baada ya mchezo huo, baadhi ya mashabiki wa soka walionekana kutoridhishwa na kiwango kilichoonyeshwa na Chama na wengine wakiamini sio yule aliyekuwa Simba kabla ya kuuzwa nchini Morocco.

 

Hata hivyo Mtemi amemkingia kifua nyota huyo raia wa Zambia akisisitiza kuwa kiwango cha Chama wa mechi Kagera ni kile kile alichoondoka nacho Simba mwaka jana.

 

“Bado yuko vizuri, hajachuja na mashabiki tutarajie pasi nzuri za mwisho na mabao kutoka kwake. Juzi alipata nafasi moja, japo viwanja vya nyasi bandia navyo huwa vina changamoto zake tofauti na vile vya nyasi halisi, vinginevyo angeweza kufunga,” amesema Mtemi na kuongeza.

 

Amesema Chama yule yule aliyeondoka ndiye yule yule aliyerudi kwenye kikosi cha Simba na hana shaka kuwa baada ya kucheza mechi tatu, nne mchango wake kwenye kikosi cha Simba utaonekana.

Leave A Reply