The House of Favourite Newspapers

Kmc Imeanza Kuonyesha Njia Sahihi Ya Kupita

0

MOJA ya timu ambayo imefanikiwa kupata mafanikio makubwa sana kwenye soka kwa muda mfupi ni KMC ya Kinondoni.

 

Timu hii ya Manispaa ya Kinondoni imekuwa ikifanya kazi kubwa sana kujipambanua na kuonyesha ni jinsi gani ni timu bora.Kuanzia wamepanda daraja mwaka 2017 imekuwa ni timu tishio sana kwenye Ligi Kuu Bara.

 

Unaweza kusema kuwa imepata kwenye mafanikio makubwa kwa kipindi kifupi labda kuliko timu nyingi kwenye ligi hiyo kwa kuwa ndani ya misimu mitatu tu wameshapata nafasi ya kushiriki michuano ya Kombe la Shrikisho Afrika.

 

Hata kama hawakufanya vizuri lakini nafikiri ni funzo kwao kuwa siku moja wanaweza kufanya vizuri kama wakifanya maandalizi mazuri ya michuano hiyo mikubwa Afrika.

KMC wamefika kwenye hadhi sasa ya kuonyesha kwanini wapo mjini, ukitazama michezo yao kadhaa ya hivi karibuni imekuwa ni timu inayocheza soka la kuvutia sana.Ukitazama mchezo wao dhidi ya Simba, Yanga na Azam utagundua kuwa ni moja ya timu ambayo imekuwa ikionyesha kiwango cha juu.Tayari wameshacheza na Simba mechi ya kwanza na kupoteza, wamecheza na Yanga moja wamepoteza na nyingine wametoka sare.

 

Hii ni tahadhari pia kwa Simba kuwa mchezo wao wa pili dhidi ya KMC hauwezi kuwa rahisi kwa kuwa ni timu yenye wastani mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa hadi sasa kwenye ligi.Ukiitazama timu hiyo ambayo kwa sasa inashika nafasi ya tano ikiwa na pointi 39 inaonyesha kuwa timu yenye malengo sahihi kwenye ligi msimu huu, labda kuliko msimu uliopita.

 

Kwenye safu ya ushambuliaji wameonekana kuwa bora kwa kuwa sasa wamefunga mabao 30, ikiwa inashika nafasi ya nne kwa mabao ya kufunga wakiwa nyuma ya Simba, Azam na Yanga.Picha halisi inaonyesha kuwa ni timu ambayo inaweza kuifunga timu nyingine yoyote kwenye ligi.

Sare ya bao 1-1 na Yanga kwenye mzunguko wa pili huku wenyewe wakionekana kuutawala mchezaji kwa sehemu kubwa inaonyesha kuwa kama kuna timu inataka kuifunga KMC basi ni lazima ifanye maandalizi ya kutosha.

 

Lakini pia pamoja na safu yao ya ulinzi bado kuna picha inaonekana kwenye safi ya ulinzi ya KMC ambayo kwenye michezo 26 waliyocheza pia wamefungwa mabao 18 pia inashika nafasi ya nne kwenye timu zilizofungwa mabao machache msimu huu ni kabla ya mchezo wa jana dhidi ya Biashara United.

 

KMC wamezidiwa na Simba ambayo imefungwa mabao tisa, Yanga imefungwa mabao 15 na Azam mabao 17.KMC wanapambana na timu kubwa tatu za Dar es Salaam, inapambana kimafanikio na Azam, Simba na Yanga.

 

Lakini pia hata kimfumo wa uendeshaji KMC wanatakiwa kurekebisha mambo machache tu lakini kiuhalisia ni kwamba wanakwenda kwenye mafanikio makubwa sana ya soka kama watakubali kuwa wavumilivu na kutengeneza timu yao taratibu.

 

Mfano idara ya habari ya KMC ni moja ya idara ambayo inaonekana kuwa bora kwa sasa, ukitaka kufahamu jambo lolote kuhusu KMC unalipata haraka tena kwa wakati, nafikiri hili ni jambo ambalo hata Simba, Yanga na Azam wanatakiwa kujifunza huku.

 

Jambo lolote la KMC ambalo vyombo vya habari vinatakiwa kulifahamu limekuwa likisambaa haraka sana na kila mpenda michezo amekuwa akilipata, hapa nafikiri watakuwa na kazi ndogo ya kuboresha.

 

Lakini pia jambo pekee ambalo KMC wanatakiwa pia kulifanya ni kutojilinganisha na Simba, Yanga na Azam kwa sasa, wanatakiwa kuendelea kufanya mambo yao taratibu na kuziheshimu timu hizo kwa kuwa zimetangulia, lakini wakiamini kuwa muda utaongea.

 

Kuingia katikati ya Simba, Yanga na Azam haiwezi kuwa kazi rahisi kwao, lakini uvumilivu unaweza kuwafanya wakafika hapo haraka.

 

Lazima KMC watakumbue kuwa wanatakiwa kujenga timu bora kwanza, yenye nidhamu, juhudi lakini pia kuwa na uvumilivu na makocha wanaoweza kuwapa jukumu la kuiongoza timu hiyo bila kuwatazama Simba, Yanga wamefanya nini?.

Leave A Reply