The House of Favourite Newspapers

KMC Wagawana Pointi Na Namungo, Ilulu

0

WAKIWA Uwanja wa Ilulu, leo Oktoba 23, 2021 Wanakinoboys wamegawana pointi mojamoja na Namungo FC kwa kufungana bao 1-1.

 

Kwa upande wa KMC ni mshambuliaji wao Charles Ilanfya alipachika msumari wa kwanza ilikuwa dakika ya 30 na lilidumu kwa muda wa dakika 12 kwa kuwa dakika ya 43 Shiza Kichuya alipachika bao kwa mkwaju wa penalti.

 

Kichuya anafikisha mabao mawili ndani ya ligi sawa na Relliants Lusajo ambaye naye yupo ndani ya Namungo FC huyu ni mshambuliaji ambaye alikuwa kwenye kikosi cha timu ya taifa kilichoshinda bao 1-0 dhidi ya Benin ugenini.

 

Mpaka mwamuzi wa kati Amina Kyando anapuliza kipyenga ngoma ilikuwa ngumu kwa milango ya timu zote mbili kutikiswa kipindi cha pili kwa kuwa mabao yote hayo mawili yalipachikwa kipindi cha kwanza.

 

Farouk Shikalo ambaye alidaka mchezo uliopita na kuokota mabao mawili mbele ya Yanga Uwanja wa Majimaji Songea leo aliokota bao moja pekee.

 

Kwa KMC nao pia walimtungua bao moja kipa namba moja wa Namungo FC, Jonathan Nahimana ambaye alitoka kutunguliwa bao 1-0 mbele ya Azam FC kwenye mchezo uliochezwa Uwanja wa Azam Complex.

Leave A Reply