Knauf Tanzania Yatoa Misaada Wilayani Kilwa
Kampuni ya Knauf Gypsum Tanzania Limited leo imekabidhi kisima cha maji kwa wakazi wa Kijiji cha Makangaga na kutoa jumla ya madawati 200 kwa shule za msingi Makangaga na Kiranjeranje zilizopo wilaya yaKilwa, mkoani Lindi.
Kampuni hiyo pia imetoa katoni 16 za pedi za kike kwa shule ya sekondari Kiranjeranje, msaada ambao utasaidia kupunguza utoro kwa wanafunzi wa kike ambao hushindwa kuhudhuria masomo wanapokuwa katika mzunguko wa hedhi.
Kisima kilichokabidhiwa kina uwezo wa kuhudumia zaidi ya watu 2,000 na kinatarajiwa kutatua changamoto ya ukosefu wa maji safi na salama ambayo ilikuwa inawakabili wakazi wa Makangaga waliolazimika kutembea umbali mrefu kutafuta huduma hiyo muhimu.
Akiongea wakati wa kukabidhi misaada hiyo, Mkurugenzi wa Knauf kanda ya Afrika Mashariki Ilse Boshoff, alisema kampuni hiyo ambayo ina migodi ya kuchimba gypsum katika vijiji husika imeamua kutoa misaada kwa wakazi wa vijiji hivyo ikiwa ni sehemu ya kurudisha kwa jamii.
“Mradi huu wa maji siyo tu utaboresha afya za wakazi wa Makangaga bali pia utasaidia shughuli za uzalishaji mali, haswa kwa wanawake na wasichana ambao hutumia muda mrefu kwenda kutafuta maji na badala yake wasichana watapata muda wa kuhudhuria masomo yao na wanawake kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi,” alisema.
Kwa upande wa msaada wa madawati alisema ni sehemu ya jitihada za kampuni hiyo kusaidia kuboresha mazingira ya kujifunzia katika shule hizo mbili.
“Tumeamua kutoa msaada wa madawati kwakuwa tunajua umuhimu wa elimu kwa maendeleo.
Kupitia madawati haya tunaamini kuwa wanafunzi wataweza kujifunza katika mazingira bora zaidi,”
Akitoa shukrani zake kwa misaada hiyo, mwenyekiti wa halmashauri ya Kilwa, Eston Ngilangwa aliishukuru kampuni ya Knauf kwa misaada hiyo na kusema msaada wa madawati umekuja wakati muafaka kwakuwa shule zilizonufaika zilikuwa zinakabiliwa na uhaba wa madawati.
Kuhusiana na mradi wa maji alisema Maji ni uhai, tunawashukuru Knauf kwa kutuletea uhai.
Wakina mama na wasichana ambao walikuwa na mzigo wa kutafuta maji kwaajili ya familia sasa watapata huduma hii muhimu jirani na maeneo wanayoishi.”