The House of Favourite Newspapers

Kocha Simba abeba mabegi, atimka

INAELEZWA Kocha Msaidizi wa Simba, Denis Kitambi, ameamua kujiondoa kwenye timu hiyo kufuatia madai ya kutopewa mkataba tangu ajiunge na timu hiyo. Kocha huyo alijiunga na Simba, Februari, mwaka huu baada ya kurejea nchini akitokea Bangladesh alipokuwa akifundisha katika Klabu ya Saif.

 

Taarifa za uhakika kutoka ndani ya uongozi wa timu hiyo, zinasema kuwa kocha huyo ameamua kujiweka pembeni na kurejea kwao mkoani Morogoro mara baada ya mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya TP Mazembe akishinikiza kupewa nakala ya mkataba wake pamoja na barua ya uthibitisho wa kazi yake.

 

Kitambi hayupo kwenye timu tangu ilivyorejea kutoka DR Congo Aprili 14, mwaka huu, aliamua kurejea kwao kwa sababu bado ana madai ya mkataba wake ambao hajapewa nakala yake na nakala ya kuthibitisha kazi yake kwa kuwa kocha Patrick Aussems aliomba kwanza mwezi mmoja wa kumuangalia uwezo wake wa kazi yake, maana hakutaka kitokee kilichotokea kwa Masoud Djuma.

 

“Unajua hadi ameamua kujiweka pembeni imeshachukua miezi miwili tangu aanze kudai kwa sababu mkataba wake aliosaini ulikuwa ni miezi minne na kila akiwasiliana na CEO (Crescentius Magori) haonyeshi dalili zozote za kumsikiliza, maana hata kocha ameshawakumbushia hadi ameona akae kimya, kwa sababu hajui kwa nini inakuwa hivyo, hivi tunavyoongea yupo kwao Morogoro kwani anaona viongozi hawapo tayari,” kilisema chanzo.

 

Championi lilimtafuta kocha huyo ambaye alipopatikana alisema kwa kifupi kuwa ni kweli hayupo na timu kwa kuwa anashughulikia mambo yake ya kifamilia kisha akakata simu. Alipotafutwa Mtendaji Mkuu wa Simba, Crescentius Magori, kwa njia ya simu jana Jumanne, alisema: “Mnanitafutia nini sasa hivi, nashughulikia mechi, mtafuteni Manara (Haji msemaji wa klabu hiyo).” Licha ya Manara kutafutwa, lakini simu yake haikupatikana

Comments are closed.