The House of Favourite Newspapers

Kwa Mwanangu Nitakayemzaa 30

0

Mtima na rafiki yake Abdulrahman wanaanzisha Kundi la Kigaidi la WAB (War Against Blacks) walilolisajili kwenye mtandao wa makundi maarufu ya kigaidi duniani wakiwa na malengo ya kulipiza kisasi kwa binadamu hasa ngozi nyeusi kutokana na unyama waliyomfanyia Abikanile, mama yake mzazi na Mtima uliochangia apoteze maisha wakati akijifungua katika Jiji la Rotterdam, Uholanzi miaka mingi iliyopita.

SONGA NAYO…

SIKU  hazikusimama, zilizidi kusonga mbele kwa kasi ya kimbunga  ambapo kwa wakati huo kila aliyekuwa anamhusu Mtima alimkatia tamaa na kuamua kuyakabidhi maisha yake mbele za Mungu huku wakisema yeye pekee ndiye aliyekuwa anaifahamu hatima yake.

“Lazima atakufa, walikuwepo watu wenye nguvu walioitikisa duniani kama akina Sadam Husein, Osama bin Laden na Moummar Gadaffi, lakini leo wako wapi?” Alile alimwambia kila mtu pale walipokuwa wanaongelea habari za Mtima.

Lakini jambo ambalo hakulifahamu, kwa kijana huyo kifo kilikuwa ni kitu ambacho hakuwa anakiogopa kabisa, alishajisemea; “Kama mama yangu alikufa lazima ipo siku na mimi nitakufa, lakini kabla sijafa lazima niwalipishe walimwengu damu ya mama kwa uhai wao.”

***

Baada ya kukacha shule na kuhama kwa Mzee Johannes Mtima na Abdulrahman waliamua kuishi mafichoni kwenye msitu wa Kirt Bell uliopo nje kabisa ya Jiji la Amsterdam, wakaanza kufanya taratibu za kusafiri hadi Afrika kuianza kazi yao hiyo.

“Tutaanzia wapi?” Mtima alimuuliza Abdulrahman kwa kuwa yeye aliifahamu Afrika zaidi yake.

“Nyumbani Somalia.”

“Sawa.”

Kwa kuwa pesa kwao hazikuwa tatizo, baada ya kufanya maandalizi siku chache baadaye kwa kutumia Shirika la Ndege la Amsterdam Airways walisafiri hadi Mogadishu, Somalia.

“Karibu Afrika kaka,” Abdulrahman aliongea baada ya kumaliza kukaguliwa katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mogadishu.

“Asante,” Mtima alijibu.

“Bila shaka utaifurahia hali ya hewa.”

“Inawezekana lakini watu wake siwezi kuwafurahia.”

“Kweli, wana roho mbaya.”

“Sana.”

Waliendelea kusogea hatimaye wakafika eneo zilikoegeshwa ndege ndogo zilizofanya safari za ndani, baada ya kupata tiketi walisafiri tena kuelekea katika Mji wa Garbaharey uliopo kusini-magharibi mwa Somalia, walifika baada ya masaa matatu wakahitimisha safari yao ndani ya hoteli yenye hadhi ya nyota tano iitwayo El- Vigia.

Siku hiyo ilipotea vijana hao wakiitumia kwa mapumziko lakini siku iliyofuata, majira ya saa kumi za jioni walitembelewa na mmoja wa viongozi wakubwa wa Kikundi cha Al- Shabaab, Mohammed Zakariyah ambaye alikuwa anafahamu kuhusu ujio wao, aliwawezesha silaha za kivita pia aliwaambia kama wangehitaji msaada wake muda wowote wangemshitua.

“Sasa kazi imeanza.” Mtima alimwambia Abdulrahman.

“Ni kweli.”

“Lakini vipi kuhusu ndugu zako.”

“Sitaki kusikia juu ya hilo, ndugu yangu ni wewe tu, walichomtendea mama yako hakikuwa kitu kizuri.

“Kweli kabisa.”

Baada ya siku hiyo vijana hao walirudi tena Mogadishi na kwenda kuweka makazi kwenye Msitu wa Aaachan, wakapanga shambulio lao la kwanza kulifanya katika Kambi ya Kikosi cha Umoja wa Majeshi ya Afrika (AMISOM), katika kambi hiyo kulikuwa na wanajeshi zaidi ya elfu moja kutoka nchi tofautitofauti Afrika na walipanga kuwateketeza wote.

***

Muziki wa taratibu ulikuwa unadunda kwenye spika zilizosambazwa kila kona ndani ya kambi ya Kikosi cha Umoja wa Majeshi ya Afrika (AMISOM) katika mji wa Mogadishu.

Wanajeshi wengi wa umoja huo walionekana kulewa kupindukia kutokana na kuwa siku hiyo ilikuwa ya mapumziko kwao, hakuna aliyekuwa anawaza kuhusu mapambano na vikundi vya kigaidi vilivyokuwa vinasumbua kwa wakati huo nchini Somalia, walikuwa wanawaza kuziburudisha nafsi zao tu.

 “Tunashambulia ndani ya dakika tano na kupotea,” Mtima alimwambia Abdulrahman kwa sauti ya chini.

 “Sawa.”

Vijana hao walizidi kuisogelea kambi hiyo ya Amisom kwa mwendo wa kutembelea tumbo huku wakiwa wameshika silaha zao mkononi zenye uwezo mkubwa kwenye mapambano ya kivita. Walivalia sare zilizofanana na zile wanazovaa wapiganaji wa Al-Shabaab. Kwa upande wa wanajeshi walizidi kula bata bila kuelewa kuwa tayari walikwishaingiliwa.

Wakiwa hawana hili wala lile mara walishangaa kuona milipuko kadhaa ya bomu ikilipuka ghafla na milio ya risasi ikirindima, wanajeshi wakaanza kukimbia ovyo huku wakiwa hawaelewi upande gani walikuwa wanashambuliwa.

Kwa upande wa Mtima na Abdulrahman, baada ya kuona wanajeshi wamechanganyikiwa walijitokeza kwa uangalifu mkubwa kisha wakaanza kuwamiminia risasi zisizokuwa na idadi kisha bila kupoteza hata nukta moja walitoweka kwa sarakasi nyingi na kuishilia kwenye Mapori ya Eq dahan.

Ukweli ni kwamba hilo lilikuwa ni shambulio la kutisha mno ambalo halikutegemewa kabisa kutokea katika siku hiyo. Kambi yote ya umoja wa nchi za Afrika, ilichafuka kwa damu na maiti! Wanajeshi wengi na watu wasio na hatia walipoteza maisha huku wengine wengi wakijeruhiwa vibaya.

Je, nini kitaendelea? Upi utakuwa mwisho wa Mtima na Abdulrahman katika maisha yao ya Ugaidi? Usikose wiki ijayo.

Leave A Reply