The House of Favourite Newspapers

Lamino Moro Achomolewa Kikosini Yanga

0

YANGA itaanza mchezo wake wa kwanza wa ufunguzi wa Ligi Kuu Bara 2020/21 bila ya beki wake wa kimataifa raia wa Ghana, Lamine Moro kutokana na majeraha ya goti.

 

Mghana huyo pia alikosa mchezo uliopita wa kirafiki walipocheza dhidi ya Aigle Noir ya Burundi, wikiendi iliyopita katika kilele cha Wiki ya Mwananchi kwenye Uwanja wa Mkapa jijini Dar es Salaam.

 

Yanga, keshokutwa inatarajiwa kujitupa tena kwenye uwanja huo kucheza dhidi ya Tanzania Prisons katika ufunguzi wa pazia la msimu huo mpya.

Kwa mujibu wa taarifa ambazo imezipata Championi Ijumaa kutoka ndani ya kambi ya timu hiyo, beki huyo hivi sasa yupo nje ya uwanja akiendelea na matibabu huku akifanya mazoezi ya binafsi kwa ajili ya kujiweka fiti.

 

Mtoa taarifa huyo alisema kuwa upo uwezekano mkubwa wa beki huyo kuikosa michezo mitatu ya ligi baada ya madaktari kushauri apumzike kwa muda wa wiki moja na nusu hadi mbili ili kuhakikisha anapona vizuri.

 

Aliongeza kuwa upo uwezekano mkubwa wa kuwaanzisha mabeki wapya wa timu hiyo, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na beki aliyevunja rekodi ya dau la usajili kwa wachezaji wazawa Bakari Mwamnyeto aliyesajiliwa kwa Sh milioni 220 akitokea Coastal Union ya mkoani Tanga.

 

“Benchi la ufundi lilianza kuwandaa mabeki wa kati Ninja na Mwamnyeto tangu awali mazoezini, hiyo ni baada ya kupata taarifa kutoka kwa madaktari kuhusu majeraha yake.

 

“Moro alijitonesha goti lake ambalo linamsumbua ambaye hatakuwa sehemu ya kikosi kitakachocheza dhidi ya Prisons.

 

“Hivyo, baada ya kupata taarifa hizo za majeraha ya Moro, benchi la ufundi likaanza kuwandaa Mwamnyeto na Ninja kwa kucheza pamoja ili wazoeane kwa kuwachezesha mchezo wa kirafiki tulipocheza na Aigle Noir ya Burundi siku ya Kilele cha Wiki ya Mwananchi,” alisema mtoa taarifa huyo.

 

Alipotafutwa Moro kuzungumzia hilo alisema: “Nilitamani sana kuanza msimu na wenzangu lakini kutokana tatizo la kiafya imenibidi nikae nje, daktari ameniambia kuwa, nitarejea hivi karibuni lakini nasubiri vipimo zaidi ambavyo natarajia kupimwa wiki ijayo.”

STORI NA WILBERT MOLANDI NA CAREEN OSCAR, Dar

Leave A Reply