The House of Favourite Newspapers

Sakata la Madini Laendelea Kuwang’oa Vigogo Serikalini (VIDEO)

0
Shehena ya Almasi ilikuwa kwenye hili sanduku.

IKIWA siku mbili baada ya Ripoti ya Uchunguzi wa Biashara ya Madini ya Almasi na Tanzanite kumng’oa Waziri wa nchi Ofisi ya Rais Tamisemi, George Simbachawene na Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Edwin Ngonyani, Waziri wa Fedha Dk. Philip Mpango ameagiza watendaji wote walioko katika Mgodi wa Almasi wa Mwadui Nyinyanga kuchunguzwa na itakapobainika wanamiliki mali zisizoelekeza wachukuliwe hatua.

Waziri Mpango  akizunguza wakati alipopokea ripoti kuhusu shehena ya almasi iliyozuiliwa katika Uwanja wa Mwalimu Julius Nyerere amesema ‘Tanzania imepigwa vyakutosha’ hivyo wale wote waliohusika katika upigaji huo washughulikiwe.

Ameviagiza vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na idara za sheria kuanza kuwachunguza wafanyakazi wa mgodi huo kama walihusika kwa njia yoyote kufanikisha utoroshaji wa rasilimali za taifa.

Amesema wafanyakazi wote wanaohusika kuanzia uchimbaji wa madini hayo mpaka kule yanakosafirishwa wamulikwe na vyombo vya dola ili kubaini uhalali wa mali wanazomiliki.

“Vyombo nataka kuanzia sasa wachunguzeni wafanyakazi ambao walishiriki katika kufanikisha kutorosha almasi zetu tena wachunguzeni kwa kina …angalieni mali zao ikiwa wana mashamba, magari, majumba, viwanja changanyeni,” amesema.

Waziri huyo ambaye kila mara alikuwa akirejea neno ‘Watanzania tumepigwa vyakutosha …Nataka Watanzania wajue mali zao’ alisema baadhi ya watumishi kwenye mgodi huo walishirikiana na wajanja wa nje kutorosha rasilimali za taifa.

“ Nasema wachunguzeni na kisha wachukuliwe hatua kuanzia wale waliopo sasa na hata wale waliokuwepo nyuma…lakini kama kuna mtu ametangulia mbele ya haki huyo basi,” amesema.

Kauli ya Waziri Mpango imekuja siku mbili tu baada ya Rais John Magufuli kukabidhiwa ripoti ya kamati iliyoundwa na Spika wa Bunge Job Ndugai ambayo ilichunguza biashara ya madini ya almasi na Tanzanite na kubaini madudu kadhaa.

Ripoti hiyo imewataja vigogo kadhaa kuhusika katika uzembe na kulisababishia taifa hasara hatua ambayo ilimlazimu Rais Magufuli kuwataka wakae pembeni kupisha uchunguzi. Juzi akizungumza na waandishi wa habari Mkuu wa Jeshi la Polisi(IGP) Simon Sirro amesema tayari baadhi ya wale waliotajwa kwenye ripoti hiyo wameanza kushughulikiwa na akawataka wengine wanaohusika kujitokeza haraka iwezekavyo..

Kuhusu almasi iliyozuiliwa katika uwanja wa ndege wa JKN, aliyekuwa mwenyekiti wa kuchunguza makinikia yanayozuiliwa katika Bandari ya Dar es Salaam, Profesa Abdulkarim  Mruma alisema thamani iliyotolewa na wasafirishaji wa mzigo huo ilikuwa ya uwongo.

Amesema kulingana na tathmini waliyofanya Tanzania ilikuwa ikipoteza mamilioni ya fedha kila mwaka kwa vile vipimo vilivyokuwa vikitumika kuthamini almasi hiyo vilikuwa haziendani na ukweli.

Akirejea yale yaliyoelezwa na Profesa Mruma, Waziri Mpango alisema kutokana na udanganyifu huo Tanzania ilikuwa ikipoteza kiasi cha 2.3 bilioni kama sehemu ya tuzo ya ada na mrahaba.  Amesema mbali na hilo kiasi kingine cha fedha kilikuwa kikipotea kutona na wajanja hao wachache kutumia njia za panya kuibia Serikali.

“Tumepigwa kiasi kikubwa kwa maana hiyo kuanzia sasa mapendekezo yote yaliyotolewa na Profesa Mruma yafanyiwe kazi na naagiza watafutwe wataalamu tena wazalendo ili kuziba mapengo yaliyopo,” amesema.

Baadhi ya maofisa wa ulinzi na usalama pamoja na taasisi ya kupambana na kuzuia rushwa( Takukuru) waliokuwepo kwenye mkutano huo walisema operesheni ya kuwachunguza wafanyakazi hao tayari imeanza kufanyika na hadi sasa wafanyakazi kadhaa walikuwa wakihojiwa.

 

Leave A Reply