The House of Favourite Newspapers

LYYN AMPASUA KICHWA TANASHA

KITENDO cha video vixen (muuza sura) ambaye ni msanii wa Bongo Fleva, Irene Louis ‘Official Lyyn’ kuonekana na mwanamuziki Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ huko Dubai katika Nchi za Falme za Kiarabu (UAE). kimempasua kichwa mwandani wa msanii huyo, Tanasha Donna, Amani limedokezwa. Lyyn ambaye ni mpenzi zilipendwa (eksi) wa Diamond au Mondi alionekana na msanii huyo nyuma ya jukwaa (back stage) kwenye Shoo ya One Africa Music Fest iliyofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita huko Dubai.

Kwa mujibu wa vyanzo mbalimbali ndani ya familia ya Mondi, tukio hilo limempa presha Tanasha katika kipindi ambacho anamlea mtoto wao wa kwanza, Naseeb Jr. Lyyn amekuwa akitupia video fupifupi kwenye kipengele cha Insta Story (IS) katika ukurasa wake wa Instagram ambapo amekuwa akijitambulisha kwa majina ya mafumbo yanayomhusu Mondi.

AJIITA SIMBA JIKE, MAMA LAO

Wakati Mondi akijiita Simba Dume, Lyyn aliibuka na kujiita Simba Jike. Wakati Mondi alipoachia ngoma yake ya Baba Lao alijipa jina hilo la Baba Lao, sasa Lyyn ameibuka na kujiita Mama Lao! Imeelezwa na vyanzo vyetu kuwa, figisufigisu za Lyyn wakati huu zinataka kumtoa roho Tanasha ambaye analea na kuishi nyumbani kwa Mondi, Mbezi-Beach jijini Dar.

Inasemekana kwamba, Tanasha anapata presha kwani anaambiwa mambo mengi na kwamba, ‘eti jamaa huyo anaanzaga’ hivyohivyo akitaka kumpiga chini mtu wake aliyenaye katika kipindi husika.

Juu ya hilo la kummwaga mwandani wake anapokuwa analea, historia ni mwalimu mzuri kwani mfano unaotumika ni wa mzazi mwenzake, Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’ mara tu baada ya kujifungua mtoto wa kiume, Prince Nillan, aliachwa na Mondi. Awali, wawili hao walijaliwa mtoto wa kike, Latiffah Nasibu ‘Tiffah Dangote’.

Kama hiyo haitoshi, mfano mwingine ni wa mzazi mwenzake mwingine, Hamisa Mobeto ambaye Mondi alimpiga ‘teke’ alipokuwa akimlea mtoto wao, Dyllan.

VITA NA TANASHA

Lyyn, kama walivyo wapenzi wengine wa Mondi waliopita, naye hafurahishwi hata kidogo kuona Tanasha kutoka nchi jirani ya Kenya anafanikiwa kuwa mke wa Mondi hivyo yupo tayari kufanya lolote kuhakikisha anaua mipango hiyo.

Gazeti la Amani linafahamu kwamba, Machi, mwaka huu, wakati penzi la Mondi na Tanasha likiwa shatashata, Lyyn alitupia picha mitandaoni zikimuonesha akiwa amelala kwenye kitanda kinachodaiwa ni cha Mondi nyumbani kwake, Madale jijini Dar kabla ya kuhamia Mbezi-Beach.

Katika tukio hilo, Tanasha alilazimika kujibu mapigo kufuatia kusambaa kwa picha na video za Lyyn akiwa amejilaza kwenye kitanda hicho huku akionekana akiwa amechoka ile mbaya. Katika maelezo yake, Tanasha aliliambia gazeti hili kuwa, siyo kila kitu kinachowekwa mitandaoni na kusomwa kinapaswa kuaminika.

Katika kufunguka huko, Tanasha alijaribu kupooza skendo hiyo kwa kuonesha kwamba kilichotokea ni kufanana kwa mazingira ya chumba na kitanda, lakini si kweli kwamba tukio hilo lilikuwa chumbani kwa mpenzi wake Mondi. Alidai kwamba, Lyyn alifanya hivyo ili kutafuta kiki na kuchafua hali ya hewa.

MONDI AFUNGUKA

Miezi kadhaa baadaye, Mondi alifunguka juu ya uhusiano wake na Lyyn pamoja na tukio hilo ambapo alisema vitanda vyao vilikuwa vinafanana kwani vilinunuliwa kwenye duka moja la fenicha lililopo Mlimani City jijini Dar na kwa kawaida vitanda vinavyouzwa kwenye duka hilo vinafanana.

Lyyn anatajwa kuwa mmoja wa mabinti walioapa kuwa na Mondi ambaye ni Rais wa Lebo ya Wasafi Classic Baby (WCB) na mara kadhaa aliwahi kusikika akitamba kuwa ndiye First Lady wa Wasafi.

Mbali na kumsababishia uhasama na mwandani wa Mondi wa sasa (Tanasha) figisu zake zinatajwa pia kumgombanisha Lyyn na wapenzi wengine wa Mondi waliopita kama Zari, Hamisa, Kim Nana na Wema ambapo hadi sasa hawako naye vizuri.

TANASHA NGANGARI

Hata hivyo, pamoja na vita nzito anayokutana nayo, Tanasha amekuwa ngangari na sasa ndiye First Lady baada ya kumzalia Mondi mtoto wa kiume na kifuatacho ni ndoa ya kihistoria. Kuna wakati Lyyn alidai kubeba mimba ya Mondi lakini baadaye iliyeyuka. Kama hiyo haitoshi, wiki mbili zilizopita Lyyn alisababisha wambeya kuibua mapya baada ya kupewa mwaliko rasmi kwenye Shoo ya Wasafi katika Viwanja vya Posta-Kijitonyama jijini Dar.

VIKUMBO NA WEMA

Mbali na hili chache zilizopita Lyyn alidaiwa kupigana vikumbo na Wema kwenye bethidei ya mwigizaji Aunt Ezekiel akidaiwa kumtumia bodigadi wake, Mwarabu Fighter kuwasiliana na Mondi ambaye naye alikuwa mwalikwa kwenye ‘iventi’ hiyo iliyofanyika Luxe Pub maeneo ya Mikocheni B jijini Dar.

LYYN MKE MDOGO?

Sasa jipya ni kujiachia Dubai, jambo ambalo limeacha minong’ono mingi kuwa huenda Lyyn akawa mke mdogo wa Mondi kufuatia kauli yake ya mwaka juzi kwamba, ataoa wake watatu au wanne.

Bado Tanasha ni mzazi, anapaswa kufuata maelekezo ya daktari na haruhusiwi kufanya kazi ngumu au kushiriki tendo la ndoa hivyo baadhi ya watu wanaamini kuwa Lyyn anataka kutumia nafasi hiyo kujitwalia umalikia.

LYYN; NO COMMENT

Gazeti la Amani liliwasiliana na Lyyn akiwa umangani (Dubai) na kumbana juu ya skendo hiyo inayomtafuna ya kujiachia na Mondi ambapo alijibu kwa kifupi; “No Comment.”

LYYN NI NANI?

Lyyn ni mrembo aliyezaliwa Buguruni, Dar, aliyeanza kujipatia umaarufu kupitia video za muziki wa Bongo Fleva kama video vixen.

Mara ya kwanza, Lyyn alionekana kwenye video ya Kwetu ya Raymond Mwakyusa ‘Rayvanny’.

Baada ya kuonekana kwenye video hiyo, uzuri wake uliendelea kumpa umaarufu mitandaoni, akajikuta kwenye skendo ya kuchepuka na Mondi wakati jamaa huyo akiwa na Zari.

Lyyn, hakusita kutangaza hadharani kuwa na Mondi kimapenzi.

Mara kadhaa, Zari akiwa hayupo Dar, alidaiwa kulala Madale kwenye kitanda cha Mondi hadi akafanikiwa kunasa ujauzito ambao baadaye uliyeyuka.

Licha ya Mondi kuachana na Zari, Lyyn aliendelea kujiweka karibu na Mondi kiasi cha kujiita Simba Jike kama vile Mondi anavyojiita Simba Dume.

MONDI AANIKA CHATI

Hata hivyo, Mondi aliwahi kutumia ukurasa wake wa Mtandao wa Instagram (Insta Stories) kuanika chati alizokuwa anafanya na mrembo Lyyn kupitia WhatsApp.

Katika chati hizo zilionesha Lyyn alikuwa akimtumia picha za mahaba akimtongoza ili amsaliti Tanasha.

Pia Mondi alionesha msimamo mkali wa kutokuwa na nia ya kumsaliti Tanasha, kwani amekua na ameacha ‘utoto’ wa kuchepuka kama alivyokuwa anafanya zamani kwa kuwa penzi la Tanasha limemtuliza.

Mondi alionesha kuchukizwa na tabia ya Lyyn, kutumia nguvu nyingi kuwaaminisha mashabiki kuwa anatoka naye kiasi cha kununua kitanda kinachofanana na chake ili tu ionekane huwa wanalala chumba kimoja.

LYYN, TANASHA

Baada ya Mondi kutoa siri ya Lyyn kulazimisha mapenzi, Tanasha alitumia ukurasa wake wa picha kukanusha chati hizo akidai kuwa ni za kutengeneza kama njia ya Mondi kujisafisha.

TANASHA PRESHA

Tanasha amekuwa upande wa Mondi, anaamini Lyyn amekuwa akitaka kumnyang’anya penzi lake na hayupo tayari kuamini kama Mondi anachepuka ndiyo maana naye alielekeza matusi mengi kwa Lyyn, lakini safari hii mrembo huyo anadaiwa kuvuruga uhusiano huo.

Stori: Sifael Paul, Dar

Comments are closed.