Maalim: Hatutasusia Uchaguzi Mwaka Huu (Picha + Video)
MWENYEKITI wa Chama cha ACT Wazalendo, Maalim Seif Shariff Hamadi amesema licha ya kuwepo kwa changamoto mbalimbali kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka huu, ACT Wazalendo hakitasusia uchaguzi huo.
Maalim Seif ametoa kauli hiyo leo wakati akizungumza na wahariri wa Kampuni ya Global Publishers baada ya kufanya ziara katika Ofisi za kampuni hiyo zilizopo Sinza-Mori jijini Dar es Salaam.
Alisema kabla ya Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Dar es Salaam kukubaliana na uamuzi wa Msajili wa Vyama vya Siasa kumtambua Profesa Ibrahim Lipumba kuwa Mwenyekiti halali wa CUF, Maalim pamoja na wafuasi wake walikuwa wameshafanya utafiti na kufahamu hatima yao kisiasa.
“Tuliunda kamati tukawaambia wapitie katika vyama washiriki wa Ukawa ili kuwauliza endapo watatupokea, na vyama vyote vilisema vitatupokea, ila waliokuwa wepesi zaidi ni ACT wazalendo ndio maana mahakama ilipoamua saa sita mchana sisi saa nane tunatangaza kwenda huko yaani ‘shusha tanga pandisha tanga’,” alisema.
“Kwa mfano wapo wanaosema tulivamia na kuchukua ofisi za matawi wakati si kweli, ni kwamba CUF ilikuwa na majengo mawili inayoyamiliki Mtendeni na Kilimahewa, mengine yote ni nyumba za watu binafsi ambao wao walitupatia nyumba zao kwa imani yao kwa CUF baada ya kuondoka wakabadili misimamo, kwamba ulipo Maalim na sisi tupo.
“Kwa hiyo hatujaenda huko kwa bahati mbaya, ukishajiunga kwenye chama hiki baada ya wiki moja unaweza kugombea nafasi yoyote, na tumeendana vizuri kabisa kwa sababu nimeshinda kwa asilimia 97 ya kura. Ado Shaibu ambaye katibu mkuu kijana kabisa kapata asilimia 100 ya kura zake. Kwa hiyo uongozi ni mchanganyiko wa zamani na wapya,” alisema.
“Naamini tutashinda kwa sababu kabla ya sisi na wenzangu kutoka CUF, ACT Wazalendo ilikuwa na matawi machache sana lakini sasa hivi Zanzibar imebadilika na kuwa purple (zambarau), CUF ukitafuta hukioni tena,” alisema.
Muda wa mabadiliko ya tume bado upo
Aidha, alisema licha ya kwamba baadhi ya watu wanadai muda wa kuibadilisha Tume ya Taifa ya Uchaguzi kuwa tume huru hautoshi, si kweli kwa sababu muda upo wa kutosha.
“ Kinachotakiwa ni kupelekea muswada wa sheria bungeni kwa hati ya dharura, tena CCM wenye wabunge wengi wanaweza kupewa maelekezo tu kuupitisha muswada huo, kwa hiyo suala la muda kuwa mdogo hatukubaliani nalo.
“ Ila hata kama hatukupata tume huru hatususii uchaguzi, sisi ni kujipanga tu kwenye uchaguzi huu. Tumemaliza chaguzi zetu ndani ya chama kazi kubwa ni kushinda uchaguzi mkuu,” alisema.
Pamoja na mambo mengine alisema muungano wa vyama vya upinzani kuelekea uchaguzi mkuu kama ilivyokuwa kwa Ukawa mwaka 2015, bado upo.
“Niseme kwamba kuna utashi kwenye vyama, kwamba tuzungumze ili tuweze kukubaliana tujifunze makosa ili yasijirudie tena,” alisema.
1
STORI: GABRIEL MUSHI, PICHA: MUSA MATEJA