The House of Favourite Newspapers

MAKAMBO ATEKA MAZOEZI SIMBA

BAADA ya straika wa Yanga, Heritier Makambo kuanza kwa kishindo, jina lake limekuwa gumzo kila kona ya Tanzania kiasi kwamba amekuwa akijadiliwa na mashabiki wote wa soka bila ya kujali itikadi ya timu zao.

 

Makambo, raia wa DR Congo, amejiunga na Yanga msimu huu na tayari ameifungia timu hiyo mabao mawili katika mechi za kimashindano alizocheza akiwa na jezi ya Yanga.

Mshambuliaji huyo alianza kuifungia Yanga bao la kwanza katika mchezo wa Kombe la Shirikisho Afrika hatua ya makundi dhidi ya USM Alger na Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 2-1, kabla ya kupata ushindi kama huo kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Mtibwa Sugar.

 

Kutokana na kasi yake hiyo ya ufungaji, mashabiki wa Simba jana waliacha kufuatilia mazoezi ya timu yao yaliyokuwa yakifanyika kwenye Uwanja wa Boko jijini Dar na kuanza kumjadili.

Championi ambalo lilikuwepo uwanjani hapo, liliwashuhudia mashabiki hao wakiwa wamekaa kwa mtindo wa kikundi wakianza kumjadili Makambo huku wakisema kiwango chake si cha kawaida.

 

Mashabiki hao walifika mbali zaidi na kuanza kumfananisha Makambo na mastraika wa timu yao akiwemo Emmanuel Okwi na Meddie Kagere, huku wakisema atakuwa msaada mkubwa kwenye kikosi cha Yanga msimu huu.

“Huyu Makambo ni mchezaji mzuri, ameanza vizuri na anaonekana anajua sana kufunga, kiwango chake ni cha juu kama Okwi na Kagere.

 

“Kama ataendelea na mwendo wake anaweza asidumu ndani ya kikosi cha Yanga, miezi sita mingi, ataondoka tu,” alisikika mmoja wa mashabiki wa Simba katika mjadala huo.

Tayari Makambo ameshageuka staa wa Yanga akiwa amecheza mechi chache tu tangu atue Jangwani akitokea DC Motema Pembe ya DR Congo.

Wengi wanasubiri kuona atafanya nini atakapoivaa Simba Septemba 30, mwaka huu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Ibrahim Mussa, Dar es Salaam

Comments are closed.