Makocha 100 Wataka Kumrithi Amunike Stars
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limeweka wazi kuwa limeshapokea zaidi ya maombi ya kazi kwa makocha 100 wanaotaka kuinoa timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, iliyokuwa chini ya kocha Emmanuel Amunike raia wa Nigeria aliyesitishiwa mkataba.
Makocha hao wameomba nafasi hiyo baada ya TFF kufikia makubaliano ya kusitisha mkataba wa Amunike baada ya kumalizika kwa michuano ya Kombe la Mataifa Afrika (Afcon) nchini Misri.
Akizungumza na Championi Ijumaa, Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidao, alisema kuwa mpaka sasa wameshapokea zaidi ya maombi ya makocha 100 wanaoitaka nafasi hiyo huku kukiwa hakuna jina lolote la kocha mzawa kwa maana ya Mtanzania aliyechangamkia fursa hiyo.
“Tumepokea maombi ya makocha zaidi ya 100 wakitaka kazi ya kuifundisha timu ya taifa, maombi ni mengi na tunayafanyia kazi kwa uangalifu mkubwa, suala la kocha anayekuja kwa ajili ya timu ya taifa tunaomba watu
watulie tutapokuwa tayari tutatoa taarifa.
“Kwa sasa nguvu zetu tumezielekeza katika mashindano ya Chan ambapo tuna kaimu kocha mkuu wa timu ya taifa lakini niwahakikishie suala la kocha mkuu ni moja ya jambo muhimu kwa taasisi na mpira wenyewe, zoezi hili tunalifanya kwa umakini mkubwa na kabla ya kuanza kucheza mechi za kufuzu za Afcon kocha atakuwa ameshapatikana, kuhusu makocha wa ndani mpaka sasa hakuna aliomba nafasi hiyo.”
Comments are closed.