The House of Favourite Newspapers

Malaika, Kiki Zingine Zinakushushia Heshima

0
Msanii wa Bongo Fleva, Malaika Exavery Clavery.

 

Asante Mwenyezi Mungu kwa pumzi uliyonipatia siku ya leo kwa kuweza tena kupata uwezo wa kuandika Barua Nzito kwa ajili ya mdogo wangu, msanii wa Bongo Fleva, Malaika Exavery Clavery.

Kama ilivyo ada, lengo kubwa la safu hii ni kukumbushana kama jamii juu ya nyendo za vijana wetu, hasa hawa mastaa ambao kwa bahati mbaya, baadhi yao wamekengeuka linapokuja suala la maadili yetu kama taifa.

Malaika, ni mmoja wa wasanii chipukizi wanaofanya vizuri katika Bongo Fleva kwa sasa na kwa muda wa miezi kadhaa, alikuwa nchini Marekani kwa shughuli zake za kimuziki.

Malaika akiwa kwenye pozi.

Katika Mtandao wa Kijamii wa Instagram, mdogo wangu Malaika aliweka picha zake zinazoonyesha sehemu kubwa ya matiti yake yakiwa nje, kitu ambacho kwa muonekano na kimaadili, ni kama vile hakuvaa kitu.

Asichokijua, Malaika ni kwamba yeye ni kioo cha jamii na unapokuwa kioo cha jamii, matendo yako yanapaswa yaendane sawia, maana kuna watu wengi wanatamani kuwa kama yeye, wanasikiliza nyimbo zake na kadhalika.

Inapotokea kioo chao kikapata ufa, tena wa kujitakia ni lazima na mashabiki nao wanapata ufa ambao ameusababisha mwenyewe.

Ninavyomuona Malaika ni msichana mzuri mrembo, hivi unajisikiaje kuvaa kinguo cha ajabu kinachoonesha sehemu ya matiti yako?

Ukirejea kwenye vitabu vitakatifu vinasema,

ukimtamani mwanamke ambaye si mke wako, ni sawa na umeshazini naye. Kwa picha ya utupu kama ile, hivi mdogo wangu, utakuwa umezini na watu wangapi kwa wao kukutamani?

Malaika, nakupenda na ninaukubali muziki wako, hasa nyimbo ya Raruararua, ni sehemu ya ‘Playlist’ yangu ambayo baada ya kazi, nikifika nyumbani hupenda kuzisikiliza.

Unadhani kwa kitendo ulichokifanya, nitatamani mwanangu aendelee kusikiliza na kuangalia muziki wa mtu ambaye hana maadili kama jamii yake inavyotaka?

Labda Malaika anaamini katika kile ambacho vijana wanasema kiki? Kwa hiyo anaona kama vile kuwa utupu ataongeza ‘antetion’ ya watu kwake. Bahati mbaya, wasanii wanaoishi kwa kutegemea hizo kiki, ni wale wasiojiamini katika ubora wa kazi zao.

Nilishangaa na kujiuliza, hivi ni wewe Malaika ambaye nimekuwa nikikufuatilia kwa muda mrefu kupitia nyimbo zako na kukuona smati, leo umeamua kujitoa ufahamu? Kweli umdhaniaye ndiye kumbe siye.

Au hicho ndicho ulichoambulia Marekani ulikoenda kufanya shoo? Unataka kuniambia hukuona kitu kingine cha kujifunza na kutuletea zaidi ya kutafuta kiki za kishamba?

Lakini Malaika hata kama ni kiki, siyo kwa mtindo huo, mbona unaweza kufanya kitu kingine kitakachokuacha salama kuliko hizo kiki ambazo zinakushushia heshima?

Hii ni aibu, kwa msanii kama wewe kufanya jambo hilo, jiheshimu mwenyewe kabla hujaheshimiwa.

Kumbuka picha kama hizo hazifutiki kwenye mitandao ya kijamii, kuna siku utataka kufanya jambo kubwa kwa ajili ya jamii, halafu utashangaa picha zako za ajabu zinaanza kusambaa. Kwa hakika utalia kwa sababu hautakuwa umejipanga.

Hata kama wazazi na walezi wako ni Wazungu Weusi, lakini kwa staili hiyo haiko sawa. Hivi kaka au mjomba wako anayeziona picha hizo anakuangalia na kukuwazia nini?

Jaribu kuangalia namna nyingine ya kujikikisha lakini siyo ya kuachia wazi sehemu ya viungo vyako nyeti.

BARUA NZITO | GABRIEL NG’OSHA | RISASI JUMATANO

Leave A Reply