The House of Favourite Newspapers

Mali za Siri za Familia ya Kenyatta Zafichuliwa

0

Familia ya Rais wa Kenya Uhuru Kenyatta, ambayo imetawala siasa za nchi hiyo tangu uhuru, ilimiliki kwa siri mtandao wa kampuni zilizofunguliwa katika maeneo yenye unafuu wa ulipaji ushuru kwa miongo kadhaa, kulingana na uvujaji mkubwa wa nyaraka za kifedha.

 

Nyaraka za Pandora – faili milioni 12 – ndio kubwa zaidi iliyovuja katika historia. Kenyatta na watu sita wa familia yake wamehusishwa na kampuni 13 zilizofunguliwa katika maeneo yenye unafuu wa ulipaji ushuru. Bado hawajajibu ombi la kutoa maoni kuhusu ufichuzi huo.

 

Uwekezaji wa pwani wa familia hiyo pamoja na kampuni iliyo na hisa na dhamana zenye thamani ya $ 30m (£ 22m), ziligunduliwa kati ya mamia ya maelfu ya kurasa za makaratasi ya kiutawala kutoka kwenye kumbukumbu za kampuni 14 za sheria na watoa huduma huko Panama na Visiwa vya Virgin vya Uingereza ( BVI) na sehemu nyingine zinazotoza kiasi cha chini cha ushuru au zisizotoza ushuru kabisa.

 

Mali hizo za siri zilifichuliwa na uchunguzi, uliochapishwa mapema Jumapili, na Jumuiya ya Kimataifa ya Wanahabari wa Upelelezi (ICIJ), Finance Uncovered , Africa Uncensored na mashirika mengine ya habari.

 

Nyaraka zinaonyesha kwamba wakfu ulioitwa Varies ulianzishwa mnamo 2003 huko Panama, ukimtaja mama wa Bw Kenyatta, Ngina, 88, kama mnufaika wa kwanza – na kiongozi wa Kenya kama mnufaika` wa pili, ambaye angeurithi baada ya kifo chake.

 

Madhumuni ya wakfu huo na thamani ya mali yake haijulikani. Mashirika ya wakfu nchini Panama hutafutwa sana kwa sababu wamiliki wa kweli wa mali wanajulikana tu na mawakili wao na sio lazima waandikishe majina yao kwa serikali ya Panama, ICIJ inaripoti.

 

Mali zinaweza pia kuhamishiwa bila malipo ya ushuru kwa mrithi.

Hakuna makadirio ya kuaminika ya thamani halisi ya mali ya familia ya Kenyatta lakini shughuli zake kubwa za kibiashara zinasheheni kampuni katika sekta za uchukuzi, bima, hoteli, kilimo, umiliki wa ardhi na tasnia ya habari nchini Kenya.

 

Mnamo 2018, Bwana Kenyatta aliambia kipindi cha BBC Hardtalk kwamba utajiri wa familia yake unajulikana kwa umma, na kama rais alikuwa ametangaza mali zake kama inavyotakiwa na sheria.

 

“Kama nilivyosema kila wakati, kile tunachomiliki – tulicho nacho – kiko wazi kwa umma. Kama mtumishi wa umma nastahili kutangaza utajiri wangu na tunatangaza kila mwaka,” Bw Kenyatta alisema.

 

“Ikiwa kuna mfano ambapo mtu anaweza kusema kuwa kile tulichofanya au kupata hakijakuwa halali, sema hivyo – tuko tayari kufika katika korti yoyote,” akaongeza.

 

Katika mahojiano hayo hayo, Bwana Kenyatta alisema alitaka kupambana na ufisadi na kukuza uwazi kuwa urithi wake. Aliahidi kushirikiana na bunge kuunda sheria ambayo itawalazimu maafisa wa umma kutangaza utajiri wao, lakini wabunge bado hawajapitisha muswada huu.

 

Viongozi wengine wa ulimwengu waliotajwa katika nyaraka za Pandora ni pamoja na Mfalme wa Jordan Abdullah II, Waziri Mkuu wa zamani wa Uingereza Tony Blair, Rais wa Gabon Ali Bongo Ondimba na Rais wa Congo-Brazzaville Denis Sassou-Nguesso.

 

Mteja nambari 13173

Haijulikani ikiwa Rais Kenyatta, ambaye anastaafu mwaka ujao baada ya miaka 10 ofisini, alijua juu ya wakfu wa Varies lakini wakati wa ufunguzi wake unaweza kuwa na umuhimu.

 

Miezi saba mapema, alikuwa amepoteza uchaguzi wa urais wa 2002 kwa mgombea wa upinzani Mwai Kibaki, ambaye alikuwa ameapa kushghulikia uhalifu wa kihistoria na vile vile kuanzisha vita dhidi ya ufisadi.

 

Wakati huo, familia ya rais anayemaliza muda wake Daniel arap Moi, rafiki wa familia ya Kenyatta alidaiwa kuhamisha pesa nje ya nchi, kulingana na ripoti iliyovuja ya 2014 ya shirika la Kroll.

 

Familia ya Kenyatta ilianzisha shughuli zake za kisiasa na kibiashara wakati wa utawala wa rais wa kwanza wa Kenya, baba ya Uhuru- Jomo. Ameshtumiwa kwa kutumia nafasi yake kujikusanyia utajiri.

 

Baada ya kifo chake mnamo 1978, Ngina Kenyatta, mkewe wa nne, alichukua jukumu muhimu katika kupanua masilahi ya biashara ya familia.

 

Katika makaratasi yaliyoonekana na BBC, Pandora Papers yanafichua kuwa mnamo 1999, Bi Kenyatta na binti zake wawili, Kristina na Anna, walianzisha kampuni ya pwani – Milrun Internatinal Limited – ambayo iliundwa katika visiwa vya Virgin -BVI.

 

Kulingana na ICIJ, Bi Kenyatta na binti zake walishauriwa na wataalamu wa utajiri wa kimataifa kutoka benki ya Uswisi Union Bancaire Privée (UBP), ambayo iliajiri Alcogal, kampuni ya mawakili ya Panama iliyobobea katika kuanzisha na kusimamia kampuni za pwani.

 

Muungano huo unasema hati za malipo kutoka Alcogal kwenda benki zinaonyesha kuwa washauri wa Uswisi waliwataja familia ya Kenyatta kutumia nambari ya “mteja 13173”.

 

Alcogal ilitoa ofisi iliyosajiliwa kwa Milrun katika visiwa vikubwa zaidi vya BVI, Tortola, na kuwapa wafanyikazi kufanya kazi kama wakurugenzi rasmi wa kampuni hiyo. Matokeo yake ilikuwa kampuni isiyojulikana kabisa ambayo haingeweza kuhusishwa na familia ya Kenyatta.

 

Kampuni hii ilitumiwa na Bi Kenyatta na binti zake kununua nyumba katikati mwa London, ambayo bado inamiliki, kulingana na stakabadhi kwenye ofisi ya Usajili wa Ardhi ya Uingereza zilizotazamwa na Finance Uncovered.

 

Mali kuu, ambayo hadi hivi karibuni ilikodishwa na Mbunge wa chama cha Labour wa Uingereza Emma Ann Hardy, sasa inakadiriwa kuwa na thamani ya karibu $ 1.3m. Msemaji wa Bi Hardy alisema mbunge huyo, “hakuwa na ufahamu kabisa” wa nani anamiliki jengo hilo.

 

“Ameshtushwa na kile uchunguzi huu umefichua na anaamini inaonyesha kwa nini uwazi zaidi unahitajika haraka,” taarifa yake ilisema.

 

Kulingana na Finance Uncovered , familia ya Kenyatta imetumia kampuni zingine zilizofunguliwa katika maeneo yenye unafuu wa ulipaji ushuru kununua mali mbili zaidi nchini Uingereza.

$ 30m kwa hisa na dhamana

Washauri wa utajiri wa kibinafsi wa UBP pia walisaidia kaka wa Bw Kenyatta, Muhoho, kuanzisha shirika la Panama linaloitwa Criselle Foundation mnamo 2003.

 

Wakfu huo ulisajiliwa kwa ofisi za Alcogal katika Jiji la Panama, na kwa jina liliendeshwa na wajumbe wa bodi kutoka kampuni ya mawakili ya Panama. Ilianzishwa kwa faida ya Muhoho Kenyatta, na mtoto wake Jomo Kamau Muhoho, kama mrithi.

 

Kampuni nyingine ya BVI ambayo Bwana Muhoho alikuwa nayo ilikuwa na thamani ya $ 30m katika hisa na dhamana mnamo Novemba 2016.

 

Utaftaji wa rekodi za umma huko BVI na Panama uligundua kuwa kampuni nyingi zilizohusishwa na familia ya Kenyatta sasa hazitumiki zingine kwa sababu ya kutolipa ada zifaazo kuendeshwa kisheria. Sio kinyume cha sheria kuendesha kampuni za siri, lakini zingine zimetumika kama njia ya kutakatisha fedha , kukwepa kulipa ushuru na utapeli.

 

Nyaraka za Pandora, hata hivyo, hazionyeshi ushahidi wowote kwamba familia ya Kenyatta iliiba au kuficha mali za serikali katika kampuni zao zilizofunguliwa katika maeneo yenye unafuu wa ulipaji ushuru.

 

Nyaraka za Pandora ni uvujaji wa hati na faili karibu milioni 12 zinazoonyesha utajiri wa siri na shughuli za viongozi wa ulimwengu, wanasiasa na mabilionea.

 

Takwimu hizo zilipatikana na Jumuiya ya Kimataifa ya Wanahabari wa Upelelezi huko Washington DC na imesababisha moja ya uchunguzi mkubwa zaidi ulimwenguni. Zaidi ya waandishi wa habari 600 kutoka nchi 117 wameangalia utajiri uliofichwa wa watu wenye nguvu zaidi duniani. BBC Panorama na Guardian wameongoza uchunguzi nchini Uingereza.

Leave A Reply