The House of Favourite Newspapers

Mastaa Hawa Wote Wamelala Selo 2017!

Emmanuel Elibariki ‘Nay wa Mitego’.

SHERIA ni msumemo! Huu ni msemo wa Kiswahili ambao ni maarufu na humaanisha kwamba hakuna mtu ambaye yupo juu ya sheria. Awe mtu maarufu au staa kwenye fani tofautitofauti, pale anaposhukiwa au kukutwa na hatia basi huwajibishwa kama ambavyo watu wengine hufanywa.

 

Hata hivyo pamoja na hayo yote, pale ambapo watu maarufu, wenye ‘interest’ na jamii na hapa ninazungumzia hasa kwa watu ambao wapo kwenye masuala ya burudani wanapojikuta matatani na hata kukamatwa na polisi kisha kulala selo au kuhukumiwa jela, huwa ni jambo linaloibua mtikisiko na kuwa gumzo kwa watu wengi.

Lulu Diva

ACHANA NA LULU ALIYEKO JELA

Hivyo ndivyo imekuwa miaka nenda rudi duniani kote na kwa upande wa mwaka huu, Kibongobongo, ukiachana na muigizaji Elizabeth Michael ‘Lulu’ ambaye yupo jela akitumikia kifungo cha miaka miwili kutokana na kukutwa na hatia katika kesi ya kumuua bila kukusudia muigizaji mwenzake, Steven Charles Kanumba, mastaa wengi mambo yaliwaendea kombo na kujikuta wakitupwa selo, kubwa likiwa ni lile sakata la kuhusishwa na matumizi na biashara ya dawa ya kulevya ‘unga’ lililoibuliwa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda;

 

Wema Sepetu.

WALIOLALA KWA  MSALA WA UNGA

Ifuatayo ni orodha ya baadhi ya mastaa ambao mwanzoni mwa mwaka huu walishikiliwa katika Makao Makuu ya Polisi ‘Sentro’ jijini Dar
kutokana na kuhusishwa katika sakata la unga, kutumia au kushukiwa kuwa karibu na watu wanaojihusisha na mambo hayo. Mastaa hao ni pamoja na Wema Isaac Sepetu, Agness Gerald ‘Masogange’ (kesi zao zinaendelea katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu), Winfrida Josephate ‘Recho’, Tunda Sebastian, Vanessa Mdee ‘V-Money’, Khaleed Mohamed ‘TID’, Petit Man, Babuu wa Kitaa na wengine wengi.

Muigizaji Elizabeth Michael ‘Lulu’.

NAY WA MITEGO

Emmanuel Elibariki ‘Nay wa Mitego’ anaingia kwenye orodha hii baada ya kulala selo siku mbili mwanzoni kabisa mwa mwaka huu baada ya kuachia wimbo uitwao Wapo ambapo ulitafsiriwa kuwa ulilenga kuwakashfu viongozi wa kiserikali na baadhi ya watu wenye majina makubwa kwenye jamii. Hata hivyo, baadaye Nay aliachiwa huru na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk John Pombe Magufuli ‘JPM’ huku akitakiwa kuyafanyia marekebisho ya mashairi ya wimbo huo, jambo ambalo hakulifanya.

 

WAPO WANASIASA

Mbali na mastaa wa muziki, filamu na mitindo, kwa upande wa wanasiasa, wengi walilala nyuma ya nondo hasa wale wa upinzani na waliotuhumiwa kwa ufisadi. Wapo waliotoka kwa dhamana lakini wengine wanaendelea kusota rumande. Haijapata kutokea katika historia ya Tanzania!

Comments are closed.