Mastaa wa Bongo Fleva, Dansi, Kukiwasha Tamasha la Biriani Festival na Coca Cola Kwanza
MASTAA wa Bongo Fleva na dansi wanatarajiwa kukiwasha kwa pamoja kwenye tamasha la Biriani Festival lililoandaliwa na Kampuni ya Coca Cola Kwanza ambapo mastaa kibao wa Bongo Fleva na dansi wanatarajia kuangusha burudani.
Akizungumza na wanahabari Meneja Masoko wa Kampuni hiyo, Anida Mbaraka amesema tamasha hilo linatarajiwa kufanyika Novemba 20 mwaka huu kwenye Viwanja vya Posta jijini Dar.
Meneja huyo amesema tamasha hilo linatarajiwa kuanza saa nne asubuhi mpaka usiku mzito huku akisisitiza wananchi kujitokeza kwa wingi kwenye tamasha hilo ili kushuhudia uhondo wa biriani hilo na coca cola pamoja na uwepo wa wakali wa Bongo Fleva na dansi kutoka Bendi ya African Stars Twanga Pepeta.
Tamasha hilo lilihudhuriwa na mastaa kibao waliothibitisha kukamua siku hiyo na ngoma zao mpya akiwemo Stamina, Baba Levo, John Makini, Lord Eyez na wengineo ambapo upande wa Bendi ya African Stars ‘Twanga Pepeta’ uliwakilishwa na mwanamuziki wake mkongwe Luiza Mbutu.
Meneja Anida amesema katika tamasha hilo kutakuwa ni muendelezo wa burudani ya kula biriani kutoka migahawa tofauti ambayo itatoa huduma hiyo kwa gharama ya chini kabisa itakayomfanya mteja wa kawaida kuweza kuimudu huku wakishushia na coca cola kwanza.
Ameendelea kusema Meneja Anida kuwa migahawa mbalimbali itakayotoa huduma kwenye tamasha hilo itawatoza wateja kiwango kidogo kabisa cha malipo ili hata mwenye kipato cha kawaida aweze kupata uhondo huo. Akilielezea tamasha hilo, Meneja Anida alisema;
“Tamasha hili ni muendelezo wa kampeni yetu tuliyoanza nayo Juni 6 mwaka huu ambapo kila Ijumaa tunatembelea migahawa mbalimbali na kufurahia na wateja kwa biriani kinywaji cha Coca Cola”.
“Tangu tuanzia kampeni hii hapa Dar tumeshaenda mikoa ya Dodoma na Mbeya na hivi karibuni tunatarajiwa kuelekea mikoa ya Tanga na Morogoro ambapo malengo yetu ni kufika nchi nzima,” alimaliza kusema Meneja Anida.
HABARI/PICHA NA RICHARD BUKOS