The House of Favourite Newspapers

Matajiri 9 Yanga Wajifungia

0

JANA siku nzima, sawa na saa 24, matajiri wa Yanga walijifungia kwenye moja ya hoteli kubwa kwa ajili ya kufanya kikao kizito cha kuweka mikakati ya kuwafunga watani wao Simba.

 

Mchezo huo wa Ngao ya Jamii, unatarajiwa kupigwa kesho Jumamosi saa 11:00 jioni.

 

Kikao hicho kiliwahusisha Kamati Mpya ya Mashindano ya timu hiyo ambayo imejaa matajiri watupu wakiongozwa na mwenyekiti wao, Rogers Gumbo, Abdallah Bin Kleb, Davis Mosha, Seif Magali, Lucas Mashauri, Injinia Hersi Said ambaye pia amekuwa akimwakilisha Gharib Said Mohammed, Harafat Haji, Hamad Islam na Pelegrinius Rutayunga.

 

Akizunumza na Championi Ijumaa, Gumbo alisema kuwa jana siku nzima walitarajia kuitumia kwa ajili ya kufanya kikao cha kamati hiyo.

 

Gumbo alisema kuwa katika kikao hicho agenda ilikuwa ni mikakati na mipango ya kuelekea Kariakoo Dabi ambayo ni muhimu kwao kupata ushindi.

 

Alisema kuwa mara baada ya kikao hicho, wataweka wazi mipango yao yote kuelekea mchezo huo mgumu ili kurejesha shangwe kwa mashabiki baada ya kuondolewa katika hatua ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

“Kwa asubuhi hii leo (jana) ndiyo ninatarajia kukutana na wajumbe wangu wa kamati ya mashindano baada ya hapo kila kitu kitajulikana kuelekea mchezo wetu dhidi ya Simba.

 

“Tumepanga kutumia siku nzima kwa ajili ya kufanya kikao hicho, kikubwa tunataka kuanza vizuri kwa ushindi katika msimu huu mpya, hivyo ni lazima tuweke mikakati mipya kuhakikisha tunafanikisha malengo yetu.

 

“Kama unavyofahamu huu mchezo siyo mwepesi kwetu na kwa wapinzani wetu kutokana na umuhimu na ukubwa wa pambano hili, hivyo ni lazima tupate ushindi na hatutaki kupoteza,” alisema Gumbo.

Wilbert Molandi, Dar es Salaam

Leave A Reply