The House of Favourite Newspapers

Mawaziri 15 tu!

0

w
Na Daniel Mbega

WAKATI uchumi wa Tanzania ni mdogo, baraza la mawaziri limeonekana kuwa kubwa na mzigo kwa taifa, tofauti na mabaraza ya nchi ambazo uchumi wake ni mkubwa, kama Marekani, China, Uingereza na hata nchi jirani ya Kenya, Uwazi Mizengwe linaandika.
Hali hiyo inamlazimu Rais Dk. John Magufuli alifyeke baraza hilo lenye jumla ya mawaziri 30 na manaibu mawaziri 26 na kuunda wizara 15 tu ili kuakisi hali halisi ya uchumi wa taifa na wananchi kwa jumla.

MagufuliRais Magufuli.

Tanzania yenye watu milioni 47.42, pato lake la ndani (Gross Domestic Product – GDP) kwa mwaka ni Dola za Marekani 49.18 bilioni (Sawa na Shs. 130.3 trilioni).

Uchunguzi unaonesha kwamba, kwa kasi iliyopo, Rais Magufuli anahitaji wizara 15 tu na kuteua manaibu mawaziri watano, ambapo pia yeye mwenyewe anaweza kuongoza wizara mojawapo kati ya hizo, hususan Wizara ya Fedha, Uchumi na Mipango.
Wizara nyingine ambazo zinapaswa kuwa chini ya Ofisi ya Rais ni Mambo ya Nje na Uhusiano wa Afrika Mashariki; Miundombinu, Uchukuzi na Mawasiliano; Utumishi, Ajira na Maendeleo ya Vijana; Mambo ya Ndani; na Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

barack-obamaRais wa Marekani, Barack Hussein Obama.

Wizara ambazo zinapaswa kuwa chini ya Makamu wa Rais ni Maliasili, Utalii, Mazingira, Maji na Umwagiliaji; Katiba, Sheria na Masuala ya Muungano; Afya na Ustawi wa Jamii; na Viwanda, Biashara na Masoko.
Ofisi ya Waziri Mkuu inapaswa kuongoza wizara sita ambazo ni Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi); Ardhi na Maendeleo ya Makazi; Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo; Kilimo, Mifugo na Uvuvi; Elimu, Sayansi na Teknolojia; na Nishati na Madini.

Naibu mawaziri wanaotakiwa kwenye baraza hilo ni katika wizara za Fedha, Uchumi na Mipango; Mambo ya Nje na Uhusiano wa Afrika Mashariki; Katiba, Sheria na Masuala ya Muungano; Viwanda, Biashara na Masoko; na Elimu, Sayansi na Teknolojia huku makatibu wakuu wakipewa majukumu ya kusimamia utekelezaji wa wizara hizo.
Kwa kuteua baraza hilo, atakuwa amepunguza mawaziri 15 na manaibu mawaziri 21 wa sasa, hivyo kuokoa Shs. 17.3 bilioni ambazo zingelipwa kwa mishahara na posho kwa miaka mitano.

Katika awamu iliyopita kumekuwepo na wastani wa wizara 30 huku manaibu mawaziri wakiwa 26 kutokana na kubadilika mara kwa mara, ambao katika kipindi cha miaka 10 iliyopita wameigharimu serikali takriban Shs. 54.8 bilioni kwa mishahara, posho na marupurupu mengine.
Hiyo inatokana na wastani wa Shs. 8 milioni kama jumla ya malipo ya mshahara, posho na marupurupu mengine kwa ngazi ya waziri kwa mwezi, lakini hauhusishi fedha zilizotumika kwa safari za mawaziri hao ndani ya nchi kukagua miradi ama nje ya nchi kwa ziara za mafunzo ambazo ziliwahusisha hata watendaji wa idara nyingine za serikali.
Aidha, kiasi hicho hakihusishi stahiki nyingine kama kiinua mgongo kinachokokotolewa, pango la nyumba (kwa mawaziri waliokosa nyumba za serikali), pensheni ya kila mwezi, posho ya hitimisho la kazi (winding-up allowance) pamoja na stahiki nyinginezo na kwa kuwa waziri ni mbunge, pia anastahili kulipwa posho nyinginezo kadiri itakavyoamuliwa na mamlaka husika.
Gharama hizo hazihusishi pia ununuzi wa ‘mashangingi’ kwa kila waziri na naibu waziri, ambayo gharama za mafuta na matengenezo ni kubwa.
Gharama ambazo serikali inawalipa watumishi wake hasa katika ngazi hiyo ya uwaziri ni kubwa wakati wastani wa pato la Mtanzania wa kawaida (per capita) kwa mujibu wa Benki ya Dunia, ni Dola 998.1 (Shs. 2.09 milioni) tu kwa mwaka, huku Tanzania ikitajwa kuwa mojawapo ya nchi maskini zaidi duniani.
Hata hivyo, kipato hicho kinaonekana kiko zaidi kitakwimu kuliko uhalisia, kwani wananchi walio wengi, hasa wa vijijini, wanaishi katika hali duni huku wakikabiliwa na ukosefu wa huduma muhimu za kijamii licha ya nchi hiyo kuwa na rasilimali nyingi.
Nigeria, ambayo inaongoza kiuchumi barani Afrika huku pato lake la mwaka likiwa Dola 534.7 milioni (Shs. 1,123 trilioni), ina jumla ya mawaziri na manaibu mawaziri 35 tu baada ya Rais Muhammadu Buhari wa nchi hiyo kuwafyeka saba na yeye mwenyewe kuongoza Wizara ya Petroli.
Nchi hiyo ina watu milioni 178.52, Marekani, ambayo pato lake kwa mwaka ni Dola 17.42 trilioni (Shs. 36,582 trilioni) na idadi ya watu milioni 351.5, inaongozwa na mawaziri 16, wakati China, nchi ya pili kwa utajiri duniani ikiwa na pato la Dola 10.4 trilioni (Shs. 21,840 trilioni) kwa mwaka na watu bilioni 1.36, baraza lake linaundwa na mawaziri 25 tu.
Baraza la Mawaziri la Marekani linahusisha Wizara ya Mambo ya Nje, Wizara ya Fedha, Wizara ya Ulinzi, Wizara ya Sheria, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Biashara, Wizara ya Kazi, Wizara ya Afya na Huduma za Jamii, Wizara ya Nyumba na Maendeleo Mijini, Wizara ya Usafirishaji, Wizara ya Nishati, Wizara ya Elimu, Wizara ya Masuala ya Wazee, na Wizara ya Usalama wa Ndani.
India, ambayo ni ya pili kwa wingi wa watu duniani ikiwa na watu 1.24 bilioni, pato lake la ndani ni Dola 2.07 trilioni, lakini idadi ya mawaziri ni 27 tu.
Nchi jirani ya Rwanda yenye watu milioni 12.1 ambayo pato lake la taifa ni Dola 7.9 bilioni (Shs. 16,590 trilioni) tu kwa mwaka, baraza lake linaundwa na mawaziri 20 chini ya Rais Paul Kagame na Waziri Mkuu Anastase Murekezi, huku wakuu wa majimbo 16 ambao wamepewa hadhi ya Waziri wa Nchi, wakiwa na jukumu la kusimamia majimbo hayo kwa bidii na kuifanya nchi hiyo ndogo kupiga hatua kimaendeleo ambapo kwa sasa uchumi wake, hadi kufikia robo ya kwanza ya mwaka 2015, umefikia asilimia 7.6.
Uingereza, ambayo ni nchi ya tano kwa uchumi imara duniani pato lake likiwa Dola 2.95 trilioni (Shs. 6,195 trilioni), ina mawaziri 19 na maspika wawili – wa Bunge la Makabwela na Bunge la Mabwanyenye – na Chancellor wa Duchy of Lancaster.
Hata hivyo, wapo wajumbe wengine nane wanaohudhuria vikao vya baraza la mawaziri, hivyo kufanya wajumbe halisi kuwa 31 tu, akiwemo Waziri Mkuu David Cameroon. Uingereza ina jumla ya watu milioni 64.77.
Baraza la mawaziri la Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya kwa sasa lina mawaziri 18 tu huku Makatibu Wakuu 26 wakiwasaidia mawaziri hao katika idara mbalimbali. Awali kulikuwa na wizara 33.
Kwa mujibu wa Katiba ya mwaka 2010 ya nchi hiyo, ambayo idadi ya watu ni milioni 45.56 na pato lake ni Dola 60.72 bilioni (Shs. 127.5 trilioni) kwa mwaka, baraza la mawaziri linapaswa kuwa na mawaziri 22, ambapo mawaziri hao siyo wabunge na wanapaswa kuomba kazi kabla ya kuthibitishwa na Bunge lenyewe.
Utaratibu huo umeondoa ukiritimba wa mtu mmoja kuwa na vyeo viwili – uwaziri na ubunge – hivyo kunusuru mapato ya serikali na kukuza kipato cha mwananchi mmojammoja kutoka Dola 1,012.9 mwaka 2011 hadi Dola 1,358.3 mwaka 2014.
Tanzania haiwezi kujilinganisha na Afrika Kusini wala Uganda, ambazo mabaraza yao yana utitiri wa mawaziri japokuwa uchumi unatofautiana.
Afrika Kusini, ambayo pato lake ni Dola 350.1 bilioni (Shs. 735.2 trilioni) kwa mwaka, baraza lake chini ya Rais Jacob Zuma lina mawaziri 35 na manaibu mawaziri 37 huku kipato cha mwananchi mmoja mmoja kikiwa kimeporomoka kutoka Dola 8,080.9 mwaka 2011 hadi Dola 6,477.9 mwaka 2014. Afrika Kusini ina watu milioni 54.
Baraza la Mawaziri la Uganda chini ya Rais Yoweri Museveni na Waziri Mkuu Ruhakana Rugunda, lina jumla ya mawaziri 33 na mawaziri wa nchi 38 kufanya jumla ya mawaziri wote kuwa 71, likiwa ndilo baraza kubwa zaidi katika Afrika Mashariki na Kati.
Hata hivyo, pato la Uganda yenye watu milioni 38.84 ni dogo kulinganisha na Tanzania ambapo kwa sasa ni Dola 26.09 bilioni kwa mwaka, huku kipato cha mwananchi mmojammoja kikiwa Dola 696.4 kwa mwaka.
Ingawa muundo wa utawala wa Marekani ni wa shirikisho (federal) ukihusisha majimbo tofauti na Tanzania, lakini, ili kuhakikisha serikali ya Rais Magufuli inabana matumizi, kuhimiza uwajibikaji na kuleta maendeleo, lazima wakuu wa mikoa wapewe majukumu ya kusimamia maendeleo katika mikoa yao huku wizara zikitoa usimamizi wa jumla kwa miradi mbalimbali ya maendeleo.
Wachambuzi wa masuala ya utawala na maendeleo wanaeleza kwamba, mipango yote ya maendeleo inaanzia kwenye halmashauri, hivyo madiwani wana jukumu kubwa la kusimamia miradi ya maendeleo pamoja na fedha za miradi hiyo.
Kwa mujibu wa utaratibu wa sasa, bajeti kuu ya serikali inaanzia kwenye halmashauri, hivyo madiwani wana wajibu mkubwa wa kusimamia miradi ya maendeleo na endapo serikali itashindwa, basi madiwani watakuwa hawakutimiza wajibu wao.
Katika kipindi hiki cha uwajibikaji, wakuu wa mikoa husika wanatakiwa wasimamie halmashauri zao kuhakikisha maendeleo yanapatikana kwa wananchi, zikiwemo huduma muhimu na bora za kijamii kama afya, maji, elimu na miundombinu.

Leave A Reply