The House of Favourite Newspapers

Mbelgiji: Vita Hawatoki Taifa Kesho

Mbelgiji, Patrick Aussems.

 

SIMBA, kesho Jumamosi inatarajiwa kujitupa uwanjani kucheza na AS Vita ambapo kocha mkuu wa timu hiyo Mbelgiji, Patrick Aussems amepanga kuutumia mchezo huo kuweka historia kwa kupata ushindi kisha kucheza Hatua ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Kauli hiyo, aliitoa juzi mara baada ya kumalizika kwa mazoezi wakiwa katika maandalizi ya mwishoni kwa ajili ya mchezo huo utakaopigwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

 

“Ni mechi ngumu kwetu kwa sababu tunacheza na wapinzani ambao walitu­funga kwao, lakini hakuna namna inabidi tushinde sasa kwa ajili ya kufika hat­ua ya robo fainali kukamili­sha kile ambacho tulikuwa tunakiwaza kila mmoja hapa,” alisema kocha huyo.

Simba itashuka uwan­jani ikiwa na hasira ya kupoteza mchezo uliopita wa michuano hiyo dhidi ya JS Saoura uliochezwa Algeria ambao ulimalizika kwa timu hiyo kufungwa mabao 2-0.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Aussems alisema kuwa mchezo huo wanauchuku­lia kama fainali ili kuhakiki­sha wanashinda.

Aussems alisema tayari amekamilisha maandalizi ya kikosi chake kuhakikisha wachezaji hawafanyi ma­kosa kama yaliyojitokeza kwenye mchezo uliopita.

 

“Mchezo huo na AS Vita wa mwisho, hivyo ni lazima tucheze kufa au kupona ili kuhakikisha tunafanikisha malengo yetu tuliyojiwekea ya kuwafunga wapinzani wetu na kutengeneza historia kubwa nchini.

 

“Na hilo linawezekana kabisa kwetu, kwani tutakuwa kwenye uwanja wetu wa nyumbani, hivyo ninatarajia kuwaona mashabiki wa Simba wakijitokeza uwanjani kwa ajili ya kuisapoti timu yao ili tuchukue pointi nyingine tatu baada ya kuzichukua za Al Ahly na JS Saoura hapa nyumbani.

“Lakini wakati tukiweka mikakati hiyo ya ushindi, tut­aingia uwanjani kwa tahadhari kubwa ya kuwahofia wapinzani wetu kwa maana ya kulinda na kushambu­lia goli la wapinzani ili Vita wasipate bao golini kwetu,” alisema Aussems.

 

Kocha Yanga aikandamiza Simba

Licha ya AS Vita ya DR Congo kupenyezewa taarifa kibao kuwa­husu Simba kutoka kwa Kocha Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera ambaye ni Mkongo mwenzao, la­kini Aussems ametamka kuwa hata iweje Vita watakufa.

Vita tayari wapo Dar baada ya kutua usiku wa kuamkia jana Alhamisi wakiwa tayari kwa ajili ya kupambana na Simba katika mechi ya mwisho ya Kundi D.

 

Wiki iliyopita Zahera aliliambia gazeti hili wazi kuwa atawapa mbinu Vita na yote anayofahamu kuhusu Simba kwa kuwa kocha wa Vita ndiye bosi wake katika timu ya taifa ya DR Congo na kwake siyo tatizo kutoa maoni yake anayofa­hamu licha ya kutambua hicho siyo kigezo sahihi kwa Simba kushinda.

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais – Mazingira na Muungano, January Makamba ndiye ambaye anatarajiwa kuwa mgeni rasmi wa mchezo huo.

Comments are closed.