The House of Favourite Newspapers

MBINU ZINAZOWEZA KUKUFANYA UKAMTEKA KIHISIA MUWAPO FARAGHA

NI Ijumaa nyingine murua kabisa tunapokutana kwenye uwanja huu mzuri, mahali tunapojuzana kuhusu mambo mbalimbali yanayohusu uhusiano wa kimapenzi na maisha kwa jumla.

 

Leo ningependa tujadiliane kuhusu mbinu za kumteka kihisia mwenzi wako muwapo faragha. Tatizo kubwa linalowasumbua watu wengi waliopo kwenye uhusiano wa kimapenzi, ni kushindwa kujua namna ya kutengeneza mazingira yatakayowafanya wenzi wao wakahama kihisia wawapo faragha na kuanza kuelea kwenye ulimwengu wa tofauti kabisa na kuyafurahia mapenzi.

 

Kama na wewe ni miongoni mwa watu ambao unapofika muda wa wewe na mumeo au mkeo kukutana faragha unatamani kama ratiba iahirishwe, unapaswa kujiuliza mara mbilimbili, unakwama wapi?

Makosa wanayoyafanya watu wengi, ni kujiona kama wao hawana tatizo ila wenzi wao ndiyo wenye matatizo. Lazima utambue kwamba mabadiliko yanaanza na wewe, kama unaona kabisa kwamba yale mashamsham yaliyokuwepo awali yamepotea kabisa mnapokutana faragha, unapaswa kuchukua hatua za haraka. Mapenzi ni ufundi na ubunifu na kila siku unatakiwa kujifunza mbinu mpya. Unatakiwa kuondoa kabisa kitu kinachoitwa mazoea muwapo faragha, kila siku jitahidi kuwa na kitu kipya kitakachonogesha penzi lenu.

MAMBO YA KUZINGATIA

Mambo muhimu ya kuzingatia kuhakikisha mwenzi wako anavutika kihisia na wewe muwapo faragha, kubwa la kwanza ni usafi. Hakikisha mwili wako unakuwa safi muda wote kabla ya kukutana na faragha.

Baadhi ya wanawake huwa wanajiremba na kujipodoa wanapokwenda kwenye sherehe au wanapotoka ‘auti’, lakini wakiwa wanaingia faragha, hawakumbuki hata kupiga mswaki au kuoga. Baadhi ya wanaume pia unakuta mtu ametoka kwenye shughuli za kutwa nzima, amechafuka, ananuka jasho, akifika hakumbuki hata kwenda kuoga, anataka kuingia faragha na mwenzake.

Haya ni makosa makubwa, hakikisha chumba kipo kwenye mandhari nzuri, mwili upo katika hali ya usafi, lakini pia hakikisha hata kauli zinazotoka kwenye kinywa chako ni zile za upole, za kubembeleza na kichwani weka nadhiri ya kutaka kumfurahisha. Ukishaitengeneza akili yako kwa mfumo huu, utakuwa umefanikiwa kupiga hatua moja kubwa kuelekea kwenye kuziteka hisia zake. Sasa baada ya kuhakikisha umeikamilisha hatua ya kwanza, hatua ya pili ambayo watu wengi huwa inawashinda, ni utulivu wawapo faragha na wenzi wao.

Ni makosa makubwa upo ndani na mwenzako, lakini mara uhangaike na simu, mara upo bize na TV! Unatakiwa kutuliza akili yako sehemu moja, muoneshe kwamba yeye ni muhimu sana kuliko kitu chochote, zungumza naye kwa uchangamfu, mpe muda wa kuwa mfalme au malkia katika himaya yako.

 

Hata kama hakuwa na hisia na wewe kwa wakati huo, ukiyafanya haya kwa mpangilio na utulivu mkubwa, hakika utaziteka hisia zake na atakuonesha ushirikiano ambao hukuutarajia. Ukifanikiwa katika hili, unatakiwa kuongeza ubunifu wa kuhakikisha kila siku unaziteka hisia zake kwa asilimia mia moja na hakika utayafurahia mapenzi.Tukutane wiki ijayo kwa mada nyingine nzuri

Comments are closed.