A-Z Mchezaji Mtibwa kuuawa kwa kisu
Jeneza lenye mwili wa marehemu John Mabula.
Stori: Gladness Mallya, Risasi Jumamosi
DAR ES SALAAM: Inauma sana! Aliyekuwa mchezaji wa zamani wa Mtibwa Sugar, John Mabula (38) na shemeji yake, Ncheye Festo (25) wameuawa kikatili kwa kuchomwa visu vilivyosababisha utumbo kutoka nje na kufariki dunia, Risasi Jumamosi lina undani kamili.
Waombolezaji wakilia kwa uchungu
Tukio hilo la kikatili lilitokea Jumamosi iliyopita katika baa moja iliyojulikana kwa jina la Kwa Mrema iliyopo Rungwe, Kitunda jijini Dar es Salaam ambapo Mabula na Ncheye walikuwa wakipata kinywaji.
John Mabula enzi za uhai wake
Akizungumza kwa uchungu mke wa marehemu Mabula, Herieth Kifai alisema siku ya tukio alikuwa na mume wake na mdogo wake ambapo katika kupata kinywaji mdogo wake Ncheye alisimama na kujikuta akiziba TV iliyokuwa ndani ya baa hiyo hali iliyosababisha mtuhumiwa wa mauaji ambaye ametajwa kwa jina la Sylivester kumjia juu na kuanza kumtukana matusi ya nguoni.
Mabula enzi za uhai wake, akipeana mkono na mbunge Prof. Maji Marefu kabla ya mechi kuanza.
Aliendelea kusema kutokana na matusi hayo mumewe John alimuuliza mtuhumiwa kwa nini anatoa matusi kiasi hicho hivyo kukawa na mabishano kwa muda na baadaye yakaisha wakahamia kwenye meza nyingine.
“Tukaendelea kunywa lakini ghafla nilimuona huyo Sylivester akitokea kaunta na kuja kwa kasi huku ameshika kisu nikamwambia mume wangu na mdogo wangu tuingie ndani tukaingia haraka, nilikuwa wa mwisho hivyo aliniwahi na kunichoma kisu cha mkononi na begani.
“Mume wangu baada ya kuona hivyo akapaniki wakaanza kupambana naye na kufanikiwa kumnyang’anya kisu cha kwanza, akatoa cha pili kwenye begi akanyang’anywa pia, cha tatu ndicho ambacho sikujua alikitoa muda gani ambacho alimchoma mume wangu tumboni na utumbo wote ukatoka nje na kudondoka chini huku mdogo wangu naye akichomwa tumboni pia japokuwa haukutoka wote.
Ni vilio, hudhuni na majonzi
“Nilitoka mbio na kwenda kuwaita majirani na mjumbe maana wakati wa vurugu watu wote walikimbia hapo baa lakini tulipofika tulikuta tayari wamefariki dunia, walichomwa visu vingi sehemu mbalimbali za mwili hivyo damu ilitoka nyingi sana, siku hiyo mume wangu alikuwa ameuza gari lake hivyo alikuwa na hela lakini hazikuonekana, muuaji alizichukua na kesho yake viliokotwa vitambulisho viwili cha kwangu na cha mume wangu pamoja na hati ya kiwanja iliyokuwa kwenye pochi yake vikiwa vimetupwa mtaa mwingine,” alisema Herieth.
Hata hivyo, Herieth aliliomba jeshi la polisi nchini kumsaidia ili mtuhumiwa apatikane kwani ana maumivu ya kuachwa na watoto watatu.
Naye Mjumbe wa Mtaa wa Sunami, Godwin Edward alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo huku akisema amesikitishwa na tukio hilo kwani tangu ahamie mtaa huo halijawahi kutokea na muuaji alionekana alikusudia kwani siyo jambo rahisi mtu kutembea na visu vingi hivyo.
“Mabula ni mtu ambaye nilikuwa namtegemea sana hapa mtaani kwangu, kiukweli nashindwa hata kuongea maana ameacha pengo kubwa ambalo halizibiki kamwe,” alisema mjumbe huyo.
Mwili wa Mabula uliagwa nyumbani kwake Kitunda na kusafirishwa kwenda katika Kijiji cha Ushushu mkoani Shinyanga Jumatano iliyopita na ulitarajiwa kuzikwa Alhamisi huku ule wa shemeji yake Ncheye ukisafirishwa kwenda Kijiji cha Manda Usimao wilayani Kwimba, Mwanza na ulitarajiwa kuzikwa Ijumaa na mtuhumiwa anasakwa kwa faili la kesi ESTK/RB/8461/2016 MAUAJI.
Risasi lilipomtafuta Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Kipolisi Ilala, Salum Rashid alisema taarifa za tukio hilo bado hazijamfikia kwani ndiyo kwanza ameripoti kwenye ofisi hiyo.