The House of Favourite Newspapers

MO ALETA MAJEMBE MAWILI HATARI

SIMBA inayoanza mashindano ya Kimataifa Novemba inataka kufanya balaa lingine kwenye usajili wa dirisha dogo linaloanza mwezi huo. Wamekaa chini na Asante Kotoko wakawaambia kwamba wanataka mastaa wao wawili waliotamba kwenye Simba.

 

Kwa mujibu wa Nana Kwasi ambaye ni msaidizi wa Mtendaji Mkuu wa Kotoko, Wekundu hao wenye kiburi cha noti za mwekezaji Mohammed Dewji ‘MO’, wamewaambia siriazi kuwa wanamtaka straika mwenye rasta, Sogne Yacouba ambaye ni raia wa Burkina Fasso na kiungo fundi Douglas Owusu mwenye mkataba wa miaka miwili.

 

Sogne ndiye aliyetupia bao la Kotoko huku Simba akifunga Emmanuel Okwi. “Viongozi wa Simba wametuambia wanamtaka Sogne Yacouba na Douglas Owusu,” Nana Kwasi ameiambia Spoti Xtra.

 

“Wametuambia muda wowote watatupigia kutuambia kuhusiana na hao wachezaji, ila kuna uwezekano mkubwa wakawasajili wote kwavile walituuliza mpaka masharti ya mikataba yao,”aliongeza Nana.

 

Owusu anayecheza nafasi ya kiungo mshambuliaji anayetokea pembeni namba 7, alionyesha kiwango katika mechi hiyo dhidi ya Simba ambaye alikuwa akikabwa na Mghana mwenzake, Asante Kwasi.

 

Kiungo huyo mwenye umri mdogo anasifika kwa kukokota mpira kwa kasi huku akipiga chenga za maudhi, kuna kipindi Kwasi alilazimika kumrukia kwa kumchezea rafu ya kimakusudi kabla ya Owusu kumruka na kupiga pasi kwa mchezaji mwenzake.

 

Pia, kiungo huyo ana uwezo mkubwa kukontroo huku akipiga pasi za visigino na zile za kawaida na kufika kwa wachezaji wenzake.

 

Kiungo huyo, katika mechi hiyo na Simba alimpa wakati mgumu Kwasi na kusababisha ashindwe kupeleka mashambulizi kutokea pembeni kwenye goli la Kotoko.

 

Katika mechi hiyo, Kwasi alipiga krosi moja pekee katika kipindi cha mwanzoni pekee baada ya kutojua uwezo wa kiungo huyo, lakini baada ya kumjua alicheza kwa tahadhari kubwa kwa hofu ya kusababisha madhara golini kwake.

 

Lakini, licha ya kucheza kwa tahadhari hiyo kuna wakati Kwasi alijaribu kupeleka mashambulizi kwenye goli la Kotoko kabla ya mabeki wa timu hiyo kufanya shambulizi la ghafla iliyomkuta Owusu na kupiga krosi safi Yacouba kujaribu kumchambua kipa wa Simba, Aishi Manula kabla ya kuupangua mpira na kuwa kona.

 

Simba wanataka kumsajili kiungo mshambuliaji kwa ajili ya kumrithi Mganda, Emmanuel Okwi ambaye awali alikuwa akicheza namba 7 akitokea pembeni kabla ya msimu uliopita kuanza kutumika kama namba 10.

Comments are closed.