The House of Favourite Newspapers

MO Dewji Aidai Klabu ya Simba Bilioni 6

IKIWA ni wiki chache tangu mchakato wa mabadiliko ya uendeshaji wa Klabu ya Simba ufikie katika hatua nzuri, imebainika kuwa tayari kuna ‘mzigo’ mrefu wa ‘mkwanja’ umeshamwagwa klabuni hapo. Kuelekea mabadiliko hayo, mwanachama wa siku nyingi wa klabu hiyo, Mohamed Dewji ‘Mo’ ndiye anayepewa nafasi kubwa ya kuwekeza klabuni hapo kwa kununua hisa asilimia 49, pindi mabadiliko yatakapokamilika.

 

Habari za uhakika ni kuwa imebainika mwekezaji huyo ameshawekeza fedha takriban kiasi cha shilingi bilioni sita kutokana na kuihudumia timu hiyo katika masuala mbalimbali, baadhi ya masuala hayo ni kambi na safari mbalimbali za kitimu ambapo kila fedha inayotoka imekuwa ikirekodiwa kwenye kumbukumbu za klabu.

Mwanachama wa siku nyingi wa klabu hiyo, Mohamed Dewji ‘Mo’

Mo ambaye kupitia moja ya kampuni zake alisaini mkataba wa kutangaza kwenye jezi za Simba kwa Sh milioni 250, anawania kununua hisa hizo kama ambavyo Simba ilipewa muongozo na serikali kisha asilimia 51 zimilikiwe na wanachama.

Kwa mujibu wa kigogo mmoja ambaye yumo ndani ya klabu hiyo, sehemu ya fedha za Mo ni zile zilizotumika
kuipeleka Simba kambini nchini Uturuki kwa wiki mbili, kuweka kambi kwenye hoteli za kifahari pamoja na kusafiri kwa ndege pindi inapokwenda kucheza mechi nje ya Dar.

 

Katika uwekezaji ambao Mo anatarajiwa kuufanya, iliwahi kuelezwa kuwa gharama za hisa anazotaka kununua ni Sh bilioni 20, hivyo kwa kiwango ambacho ameshatoa hadi sasa ni kama tayari ameanza kupunguza kiasi ambacho atatakiwa kuwekeza kwa kuwa inahesabika kuwa ni deni.

 

“Kila kitu kinachotolewa na Mo kwa sasa Simba kinakopeshwa kuanzia kambi ya Uturuki, safari za ndege na kambi za hapa nyumbani na kila kitu ambacho kinatolewa kinakuwa kinaorodheshwa na mwisho wa siku kinalipwa na si kama anajitolea. “Kinachofanyika hivi sasa ni kama ilivyo kwa Yusuf Manji alivyofanya kwa Yanga ambapo aliikopesha na baadaye alikuwa akidai fedha zake.

 

“Fedha hizo zinatarajiwa kulipwa kupitia Sh bilioni 20 ambazo ataziwekeza, hadi sasa bado hazijawekwa hadi hapo baadaye, hivyo kila kinachofanyika kinajumlishwa kisha kinafidiwa katika fedha hizo,” kilisema chanzo hicho. Aidha, Championi Ijumaa lilimtafuta Kaimu Rais wa Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’ azungumzie suala hilo lakini simu yake imekuwa ikiita bila ya kupokelewa

Comments are closed.