The House of Favourite Newspapers

Mshambuliaji Cesar Manzoki Kutua Simba na Mambo Matatu Dirisha Dogo

0
Mshambuliaji wa Dalian Professional ya China, Cesar Manzoki.

WAKATI Klabu ya Simba ikielekea kwenye uchaguzi mkuu Januari 29, 2023, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Simba, Salim Abdallah ‘Try again’ ameibuka na kutaja mambo matatu muhimu klabuni hapo ikiwemo usajili wa mshambuliaji wa Dalian Professional ya China, Cesar Manzoki.

Mwanzoni mwa msimu huu, iliripotiwa kwamba, Manzoki amemalizana na Simba kwa ajili ya kuichezea timu hiyo, lakini usajili wake uliingia doa kutokana na timu yake ya awali ya Vipers kuweka ngumu, hali iliyowafanya kumpeleka China kujiunga na Dalian Professional ambapo mkataba wake unamalizika Desemba 31, mwaka huu.

Try Again ametoa ufafanuzi wa mambo hayo matatu ikiwemo usajili watakaoufanya katika dirisha dogo kuelekea hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

Kiongozi huyo wakati akifafanua mambo hayo kupitia akaunti yake ya Twitter, aliambatanisha na picha ambayo ina watu watatu, lakini haioneshi vichwa vyao.

Uchunguzi uliofanywa na Spoti Xtra kuhusu picha hiyo, imebainika kwamba miongoni mwao ni Manzoki akiwa katikati kutokana na michoro yake ya mkononi ‘Tatoo’ kuonekana.

Try Again alibainisha kwamba: “Wanasimba katika kipindi hiki ‘focus’ yetu ni kuimarisha benchi la ufundi liwe bora zaidi, kufanya usajili bora na sahihi, na wa nguvu ili kuiboresha timu yetu iweze kuwa tayari kupambana kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika na pia kuendelea kupambana kwenye ligi kuu ili tuchukue ubingwa.

“Kufanya uchaguzi huru na wa haki ili kupata viongozi bora wa kuiongoza klabu yetu. Naomba wapenzi na wanachama tupuuze porojo za wasioitakia mema klabu yetu. Simba ni imara na salama na itabaki kuwa hivyo daima. Simba NguvuMoja.”

Kauli ya Try Again, inakuja siku chache baada ya Mtendaji Mkuu wa Simba, Barbara Gonzalez kutangaza kujiuzulu nafasi yake hiyo aliyodumu kwa takribani miaka miwili.

Ikumbukwe kuwa, Simba ambayo inapambana kuboresha kikosi chao, pia ipo kwenye mchakato wa kusaka kocha wa kusaidiana na Juma Mgunda ambaye alikabidhiwa kikosi hicho alipoondoka Zoran Maki, Septemba, mwaka huu.

STORI: WAANDISHI WETU, SPOTI XTRA

YANGA, SIMBA ZITATOBOA MAKUNDI, NABI APEWA RUNGU, SIMBA KICHEKO | KROSI DONGO

Leave A Reply